Tuesday, June 20, 2017

IMELETWA KWAKO NA SIMULIZI MIX ENTERTAINMENT

MWANDISHI: ZUBERY RAZUUR MAVUGO.

SEHEMU YA TATU.

ILIPOISHIA:

Macho ya wapita njia pamoja na wafanyabiashara waliyokuwa eneo lile walijikuta

wakikumbwa na mshangao, wapo ambao mishangao yao iliambatana na kuwaita mama zao, lakini

pia wapo waliyomuita Mungu wao. Kufumba na kufumbua mwili wa mtoto yule ulikuwa

nyang’anyang’a huku akionekana kusumbuka kama kuku aliyekatwa kichwa. Lahaulah! Gari

lililofanya kazi ile ya kumpitia lilibakiza vumbi tu wala lisijulikane lilipoelekea.

Masikini!

ENDELEA... Watu waliyokuwa pembezoni ilibidi wamsogelee na kumzunguka. Hata

walipomfikia kwa ajili ya kufanya utaratibu wa kumpeleka kwenye kituo cha tiba, tayari walikuwa

wamechelewa. Damu nyingi sana zilikuwa zimemtoka na uhai ulimuondoka palepale. Hata

walivyo hakiki, iligundulika hivyo.

Maduhu katika harakati za kumtafuta kaka yake iliaweze kumpatia habari za msiba wa baba

yao, alijikuta akipita eneo lile la tukio. ‘’Mbona watu wengi sana pale’’ Alijisemea, kisha

akajiongeza kusogea walau kutupa jicho lake. Hata alipofika aliisikia minong’ono ya raia kuhusu

jambo lililokuwa limetokea. Naam, hakujali, akaanza kujisukuma ndani ya kundi la watu

waliyojaa ili aweze kumtazama huyo aliyepata ajari. Hatimae alifika akautazama mwili wa mpata

ajari. Ulikuwa umelala chini, damu zikiwa zimeusaliti. Ingawa mwili ule ulikuwa ni mgumu

kutambulika, lakini yeye hakushindwa kumjua kaka yake kwanzia mavazi ya juu hadi yale ya

chini. Ikabidi ahakiki.

Hakuamini macho yake. Yaani mtu anaye mtafuta kumbe nayeye tayari ameshakufa? Akawa

kama amechanganyikiwa kidogo, misiba miwili kwa pamoja. Akatoka mbiombio kama mwehu

hadi nyumbani kwao kwa ajili ya kwenda kumjuza mama yake. Njia nzima alikimba huku akilia.

Hata alipofika alimkuta mama yake akiendelea kulia ingawa macho yalikuwa yamemvimba, sauti

imemkimbia.

Akamuomba mama yake amfuate mbiombio.

‘’ Twende wapi, mbona hivyo Maduhu?’’ Mama alihoji lakini mwana hakusema chochote

zaidi ya kumlazimisha mama yake waende. Wakaianza safari mbiombio, ndani wakiiacha maiti ya

baba yake.

Hawakukawia sana kufika. Tayari Maduhu alimuonesha sehemu ambayo ilikuwa ina rundo

la watu.

‘’Kuna nini kwani?’ Mama alihoji.

‘’ Sogea uone’’ Maduhu alijibu.

Mama yule akasogea eneo lile. Hata macho ya mama yule yalipofanikiwa kumtazama mtu

aliyekuwa amelala chini huku damu zikiwa zimetapakaa kwanzia mwilini mwake hadi pembezoni

mwa mwili wake, alimtambua mtoto yule. Hakuwa mwingine bali ni mwanae Shukuru; mwanae

ambaye muda si mwili alikuwa mzima akitembea na kuongea kama kawaida. Ni mwanae

huyohuyo aliyehusika kuwafanya wapate chakula muda si mrefu sana, iweje muda huo auone

mwili wake ukiwa pale chini tena katika hali ya kutisha kama ile?

Ni kweli, mwili wake mzima ulimsisimka, mapigo ya moyo yalimwenda mbio kuliko

kawaida. Hapo akajikuta anashindwa kuvumilia, msukumo wa damu ukamuijia ghafla palepale

akajikuta akianguka chini.

‘’ Mama... Mama...maaamaaa...’’ Mwanae akabaki akiita. Raia waliyokuwa pembezoni

walishuhudia tukio lile. Wakashauri apelekwe hospitali. Harakaharaka taksi ikaitwa na mama yule

akabebelewa hadi hospitali kwa ajili ya matibabu.

Hata walipomfikisha, hakuna walichofanikisha, tayari mama yule alikuwa ameshaiaga

dunia. Hakukuwa na kingine kilichosababisha isipokuwa msukumo wa damu uliyoletwa na

mawazo mengi yaliyopitiliza. Masikini! Mtoto mdogo Maduhu akashindwa nini afanye.

Alijiona asiyependwa na mwenyezi Mungu. Misiba mitatu yote imemtokea yeye tena kwa

siku moja? Akashindwa hata nini afanye, muda wote alikuwa wa kulia tu.

Hata hivyo, wananchi wenye mioyo ya upendo na wenye utambuzi wa neno matatizo,

waliweza kushirikiana na maaskari kuhakikisha miili yote mitatu inastirika vyema. Hata

walipomaliza, hakukuwa na yeyote aliyeonesha kumjali tena mtoto yule. Kila mmoja alionekana

kuwa na matatizo kama yeye, hivyo hakuna msaada aliyoupata zaidi ya kupatiwa pole nyingi tu.

Lakini pia hawakumwacha hivyohivyo mtoto yule, walimchangia vijisenti kwa ajili ya kumsaidia

kujikimu. Walipomaliza walimwacha peke yake, naye hakuwa na pakwenda zaidi ya palepale

alipokuwa akiishi na wazazi wake. Alibaki nyumbani kwao huku akiwa amejikunyata, watu

wachache wakipita nje na kumpatia pole. Muda wote wa upweke wake mawazo mengi sana

yalimpata hofu kuu lilimwelemea kila sekunde.

Alikaa nje ya nyumba yao mpaka usiku ulipoiingia, hatimae aliamua kuingia nyumbani kwao

iliaweze angalau kupumzika. Alipofika, alikikurubia kitanda kidogo sana kilichoweka godoro

lililoishaisha. Mwili wake ukawa juu ya godoro hilo na kuulazimisha usingizi ingawa alikuwa na

hofu muda wote.

Usingizi wa visa ulimpata; usingizi uliyoambatana na njozi za kutisha hswahaswa. Ati,

anaota jitu lisilo na jina lakini lenye sura mbaya likimfuata na kumuita huku likiiomba roho yake,

mdomoni mwake likitoa kicheko cha kejeli. alijitahidi sana kukimbia lakini kila alipojaribu

kukimbia hata miguu haikuweza kukimbia, ni kama alikuwa na sumaku miguuni. Jitu lile lenye

kucheka kwa kejeli, lilimsogelea na kumfikia, likisema, ‘’ Lazma uwafuate ndugu zako.’’ Huku

sauti yake ikiambatana na mwangwi. Mh! Lilichomoa kisu ambacho hata hakikujulikana

lilipokuwa limekificha. Hapo sasa likataka kumchoma. Ni kama hakuweza kuivumilia ndoto ile ya

kuogofya, ni kama hakuweza kukubali lile jitu liyatoe maisha yake. Akakurupuka kutoka

usingizini hapohapo huku akihema utadhani mtu aliyekimbizwa.

Uoga ukamjaa, hata kukaa ndani ya nyumba yao akashindwa, mawazo yake yakawa yanamtuma

wazazi wake pamoja na kaka yake wamo ndani mule, wakimwita na kumtaka. Pengine ni utoto

ama hofu ya kuondokewa, hata hivyo hakuweza kuvumilia kuitwa, ikabidi atoke nje. Tayari usiku

ulikuwa ni wa saa saba. Hata huko nje, hali ya woga iliendelea kumsumbua. Ingawa kuna wakati

alijua ni mawazo tu yanayomsumbua lakini hakuweza kuyavumilia pia, alitamani angalau awe

katikati ya kundi la watu iliawe na ujasiri dhidi ya jambo lile lililokuwa likimsumbua akili.

Usiku ule akaanza kutembea mtaani wala asijue wapi anaelekea, ndani ya moyo wake

alimuomba mwenyezi Mungu walau giza lile liondoke na mchana uingie iliamani imrejee.

Akiwa katika pitapita zake yeye pamoja na woga wake mara kwa bali alisikia sauti ya miziki.

Bila shaka huko miziki ilipokuwa ikitokea kulikuwa na jambo fulani lililokuwa likiendelea.

Akaongeza hatua za miguu yake kuelekea eneo ambapo sauti zile alikuwa akizisikia. Muda kidogo

alifika.

Kwa mara ya kwanza akaipata furaha ndogo ndani ya moyo wake, na hiyo ni baada ya kugundua

kumbe sehemu ile kulikuwa na watu waliyokuwa wakiserebuka huku wengine waliyowazunguka

wakiwatazama kwa furaha. Akajichanyanya na muda kidogo akagundua kumbe sehemu ile

kulikuwa na mkesha wa harusi. Akamshukuru sana menyezi Mungu na hapo akajikalisha karibu

na spika zilizokuwa zikitoa mkito wa nguvu. Alifanya hivyo ikiwa ni njia yake ya kuikimbiza

hofu aliyokuwanayo. Akiuambia moyo wake pamoja na nafsi, ‘’ Ondoeni shaka, msiogope hivi

sasa tupo watu wengi’’ ingawa mbu walimfanya chakula, lakini hilo hakulijali hata kidogo,

aliuchukuwa mkono wake na kujiwasha makofi sehemu mbalimbali ambazo mbu walimuuma.

Dakika kadhaa mbele hakuwa tena akijielewa. Alikuwa katika usingizi mzito. Usingizi ule

haukuwa na mauzauza hata kidogo, ingawa alilala mbu zikimuuma lakini alikuwa na uhuru wa

nafsi yake.

‘’ Wewe mjinga. Amka, mpuuzi wewe.’’ Sauti moja ilisikika na hata kumfanya mtoto yule

afumbue macho yake kutazama. Mh! aligundua kuwa, tayari asubuhi ilikuwa imeingia, ingawa

macho yake yalikuwa bado usingizini. Katika mtazamo wake, ni kama kulikuwa na watu kadhaa

waliyomzunguka eneo lile, lakini hakujali kutokana na usingizi aliyokuwanao ambao alikuwa

akiulazimisha umtoke.

‘’ Unadhani ni nani? Nd’o huyuhuyu choko aliyetuibia... Kwani nani mwingine.’’ Sauti

nyingine ilisikika ikikoroma. Mara ngumi moja ya kichwa ikatua mwilini mwa Maduhu, maumivu

yakaandamana na kilio cha nguvu kutoka kwake. Hajakaa sawa, mara akapokea kofi la uso,

kutoka katika mkono uliyoshiba kimazoezi. Akiwa katika sintofahau, mara akahisi kama harufu

fulani ya damu. Pakepale pua zake mbili zikaanza kutoa damu. Hakupata muda wa kuuliza
ama kujiuliza ni kipi alichokosea hadi kipigo kimuangukie?

ITAENDELEA....

USIKOSE MWENDELEZO WA  HADITHI HII NZURI KUJUA NI HAPA HAPA KUJUA NI MAISHA GANI HUYU MTOTO ALIYAPITIA NA NINI ILIKUA HATIMA YA MAISHA YAKE IKIWA NDO KABAKI MWENYEWE NA NI ANA UMRI WA MIAKA SABA TU..

0 comments:

Post a Comment