Thursday, June 22, 2017

IMELETWA KWAKO NA SIMULIZI MIX ENTERTAINMENT
MWANDISHI FRANK MASAI
SEHEMU YA TANO

ILIPOISHIA

 "Lakini Mkuu, mkumbuke huyu Lobo si mtu wa kuchezea. Na mbaya zaidi tunahisi humu ndani kuna vibaraka wanaosaidiana naye. Huoni kama tutakuwa tunaiuza familia ya Mubah kwa bei rahisi kabisa." Lisa alikuwa ofisini kwa mkuu wake baada ya kutoka kwenye ule mkutano mfupi.  Alienda katika ofisi ile ili kumpa ushauri kama huo Bwana Malocha.

ENDELEA
"Usijali Lisa. Hilo pia nimelifikiria kwa kina na ndio maana pale mkutanoni, nimesema sehemu ambayo tutaificha familia ya Mubah. Lakini kiukweli, sipo huko ambapo tutawapeleka. Wataenda sehemu nyingine kabisa." Malocha alimtoa wasiwasi Lisa huku akimpa vipande baadhi ambavyo walivifanya katika ule mkutano wao.
"Okay. Hapo sawa. Na kingine tukumbuke kuwa yule pia ni Sniper, nadhani unakumbuka sana alichokifanya nyuma. Tuwe makini zaidi tukiwa maeneo ya mtaa ule. Kila baada ya kilometa mbili, kuwe na mlinzi juu na chini. Hiyo itasaidia sana."
"Usijali Lisa, nimekuelewa na nitafanyia kazi hilo." Malocha alionesha shukurani zake kwa Lisa ambaye baada ya kutoa ushauri huo, alitoka ofisini mle na kuelekea kwa Mubah ambapo napo alikuwa anamtia moyo na kumueleza mikakati waliyoipanga.   
****
Saa tatu asubuhi, yakiwa yamebakia masaa kuna na matano ili ahadi aliyotoa Lobo itumie, gari moja nyeusi ilisimama nje ya nyumba moja kubwa kiasi na baada ya sekunde kadhaa, alishuka kijana Mubah na kuelekea katika nyumba hiyo.
Katika shirika la siri la kipelelezi, sehemu ambayo Mubah anafanyia kazi, si ruhusa kwa mfanyakazi yeyote kutoka ndani ya shirika hilo mida mibaya hasa usiku. Na ndio maana hata Mubah alipopokea simu ya matatizo ya familia yake, hakuondoka hadi asubuhi hiyo ambayo kwake ilikuwa kama mwaka kuifikia.
"Oooh! Mubah. Ulikuwa wapi mwanangu." Mama yake Mubah ambaye alionekana wazi uzee umemchukua, alimkimbilia kwa shida mwana wake kabla ya familia nzima nayo haijafanya hivyo.
"Usijali mama. Nipo salama kabisa na nimekuja kwa ajili yenu." Mubah aliwapa moyo ndugu na familia yake.
"Jana alikuja mtu anaumwa, akamuomba wifi amsaidie kutibu majeraha. Sisi tulikuwa tunamwogopa, ila akasema anafahamiana na wewe. Na hata baadae alipopiga simu, tukasikia sauti yako. Sema akaenda kuongelea nje na baada ya kurudi alimuomba wifi afanye alichokiomba mwanzo. Yaani amtibu yale majeraha." Dada wa Mubah alitoa taarifa ambazo kwa Mubah alibaki akiwa kakodoa macho tu. Ye' alidhani Lobo alikuja na kuitishia amani familia yake, na kumbe alikuja kwa njia za kiutu.  Akakuna kichwa chake kijana huyu huku akishindwa afanye nini kwa wakati ule.
"Pia alipoanza kuondoka aliacha ujumbe ule pale." Dada wa Mubah alisonta kidole chake ukutani na kuonesha ujumbe aliouacha John Lobo.
Alisogea karibu maana ni kama alikuwa hauoni japo ulikuwa na maandishi makubwa meusi kwenye karatasi nyeupe iliyochomwa kwa kisu kwenye ukuta huo wa nyumba iishiyo familia ya Mubah. Ujumbe ulisomeka "TICK TOCK" na kwa juu yake saa ya ukutani ya Mubah ilikuwa ikienda taratibu kwa mlio huo wa tick tock. Mubah akahisi kuchanganyikiwa.
"Anko. Anko yule mwingine kanipa hii hapa na ......" Kabla ya yule mtoto wa dada yake, mtoto mwenye umri wa miaka saba hadi nane hajamaliza kauli yake, Mubah tayari alimpora kile kitu ambacho alikuwa kakishika yule mjomba wake. Kilikuwa ni kibanio kizuri cha nywele kilichonakishiwa na madini ghali ya dhahabu.  Mjomba yule wa Mubah alikuwa anafuraha kila alipokiangalia, lakini kitendo cha Mubah kumpora na kuanza kukikanyaga kanyaga, kikafanya yule mtoto asiseme kitu kingine ambacho kapewa. Alikuwa kavaa pambo zuri katika nkono wake, pambo hilo pia alipewa na John Lobo.
Mjomba wa Mubah akakimbilia chumbani kwa mama yake na huko safari ya kilio ikachukua nafasi yake. Aliona kama Mjomba wake kamkatili sana nafsi yake kwa kile kitendo. Watoto bwana.
"Naomba mjiandae. Leo saa mbili usiku tutaondoka katika nyumba hii. Tupo katika hatari kubwa sana. Na ninaomba, jirani au mtu yeyote asijue ni wapi au muda gani tunatatoka hapa. Tupo katika hatari." Mubah akiongea huku uso wake ukiwa na mashaka makubwa sana hali iliyofanya familia yake kuzingatia maneno yake. Familia nzima ilimjua Mubah kama askari wa Tanzania. Hivyo aliposema maneno hayo, kila mmoja akaamini kuna kitu cha hatari hasa pale walipovuta sura ya yule mtu aliyekuja usiku wa jana yake.
"Usiwe na wasiwasi dear. Mambo yote tutayafata." Ilikuwa ni sauti ya Zakia Bin Ashib ikimfariji mpenzi wake walipokuwa chumbani wakipanga baadhi ya vitu vyao kwa ajili ya kuondoka usiku huo. Maneno hayo ya faraja, yalikuja pale Mubah alipomueleza mkasa mzima uliomsibu siku ya jana yake tangu alipoanza kukimbizana na Lobo hadi unyama alioufanya kule FISSA.  Ndani ya maongezi hayo, Mubah hakuthubutu kuongea kuhusu ndege iliyoibiwa au mahali ambapo anafanyia kazi.
Zakia Bin Ashib, kila kukicha alikuwa anamuomba mpenzi wake amueleze ni wapi anafanyia kazi zake, lakini Mubah alikuwa anakataa kusema ukweli kwa sababu ya masharti ya shirika lake.
****
Saa mbili usiku, kwa kutumia handaki dogo lililo katika sebule la Mubah, familia yote iliingia huko na kutokezea katika zizi la ng'ombe, kilometa kadhaa kutoka kwenye nyumba ya Mubah. Hakuna aliyewahi kufikiria kuwa nyumba ya Mubah inahandaki hilo. Awe mama yake au mchumba wake. Hivyo kitendo cha wao kuingizwa huko na kutokea kwenye zizi la ng'ombe, likawa ni hadithi nyingine ya kusisimua ambayo Mubah alipaswa kuilezea.
Baada ya kuibukia zizini huko, gari moja ya kimarekani, ilifunguka milango yake na watu idadi ya familia ya Mubah, walijitojeza. Macho ya familia ya Mubah ikazidi kushangazwa hasa wale watu wanavofanana nao.
Watu wale, wakaipita familia ya Mubah na kuingia katika handaki lile lile ambalo walitokea familia ile. Familia ya Mubah, ikapanda na gari ile na safari ya kwenda pasipojulikana ikachukua nafasi yake wakati huo Mubah alirudi nyumbani kwake na kuanza kutoa maelezo yote yanayofaa.
Huko nje ulinzi ulikuwa ni wa hali juu kuliko hata ule ambao huwekwa rais wa nchi fulani akifika nchini. Wapelelezi walikuwa wakipita katika mtaa huo kama wapita njia na hakuna ambaye alihisi kuwa wale ni wapelelezi. Wadunguaji (Snipers) walikuwa kila upande katika eneo lile wakiwa na bunduki zao maalumu kwa ajili ya kudungulia mtuhumiwa wao.
Huko FISSA, Lisa na Malocha walikuwa wanawapa taarifa watu wao wa kazi hasa kwa picha ambazo zilikuwa zinatumwa kwa satellite. Kila mtu tofauti waliyemtilia mashaka akipita, FISSA walitoa taarifa kwa kikosi kazi chao kilichoongozwa na Mubah.
Hatimaye zikabaki dakika kumi na tano za ahadi ya Lobo kutimia. Kila mtu moyo ukawa unamdunda kwa sababu mtu wanayemtega si mtu mdogo. Ni eidha wamkamate hai au akiwa maiti. Lakini je!? Uhakika wa kumkamata upo? Swali hilo ndio likafanya mioyo ya wachapakazi wale kutokuwa na amani.
Mbwa wasiojua kubweka bali kufanya kazi yao, nao wakawa wananusa kila sehemu walipopitishwa. Ulinzi ulikuwa mkubwa haswa. Mtaa mzima anaoishi Mubah ulitapakaa ulinzi wa hali ya juu.
Zikiwa zimebaki dakika saba za jambo alilopanga Lobo kutimia, simu ya Mubah ilianza kuita mbele ya familia yake ile mpya. Namba ya mpigaji haikuonekana bali kuandika neno 'private call'.  Mubah akawapa ishara wale watu waanze kutimiza maadhimio waliyoyapanga.
Bila kuchelewa, meza kubwa ya mle ndani ikafunuliwa na watu wote wakasogea pale mezani na kutazama mahanjumati na mapochopocho kadhalika yaliyoandaliwa kiufundi na wafanyakazi wa FISSA. Wakaanza kusali kwa sauti na ndipo Mubah akasogea pembeni kidogo na kupokea simu ile.
"Hallow." Mubah akaita baada ya kupokea simu.
"Heloo Mubah. Niambie kamanda wangu." Sauti ya Lobo iliitikia upande wa pili na wakati huo wale waliondaliwa kupambana na Lobo, walizidi kupamba moto kuombea chakula.
"Stupid Lobo." Mubah akatoa tusi dogo.
"Mmmh! Siku hizi mmeokoka Mubah. Mnasalia chakula kwa kukemea kwa jina la Yesu. Muislamu halisi kama wewe!?" Lobo aliongea na kucheka sana na hapohapo wale washirika wa Mubah walikatisha sala zao na kugundua kuwa walikuwa wanasali Kikristo wakati familia ya Mubah ni Waislam. Japo Mubah alikuwa mbali nao, lakini wao pia waliyasikia yale maongezi kwa kutumia vinasa sauti vilivyokuwa masikioni mwao kama vishikizo. "Okay. Ondoa shaka Kamanda, siwezi kuingilia maisha uliyoyaanza na familia yako ya kujibambika.
Nipo hapa kukukumbusha kuwa zimebaki dakika tano na sekunde kadhaa ili ahadi yetu itimie. Huku ulipoileta familia yako, nadhani panafaa sana kufanya kazi yetu. Na kingine, kabla sijafanya chochote kwa huo ugeni ulioniletea kwako, naomba utoke nje na ushuhudie mara ya mwisho mtaa wako. Toka, waweza kuniona navyoua vimbwa vyenu." Lobo akamaliza kuongea lakini hakukuta simu.  Mubah akawa kama kachanganyikiwa, akatoka nje kasi na kuanza kuangaza huko na huko, akasogea hadi barabarani na kuzidi kushangaa. Aliweza kuwaona wapelelezi wenzake na wakamuoneshea ishara ya kumuuliza vipi? Lakini Mubah ni kama alikuwa kapandwa na kichaa na wakati huo simu ikiwa sikioni kwake.
"Ha ha hahahaaa. Mubah, Mubah, Mubah. Bado dakika mbili. Embu ongea kwanza na mjomba wako." Lobo alisikika tena kwenye simu ile aliyoipiga.
"Ankoo tusaidie tumefungwa kamba na jambaziii." Mjomba wa Mubah alipiga kelele kwa nguvu na kumfanya Mubah ahisi kama anamabawa lakini hawezi kupaa kwenda kutoa msaada. Akabaki katikati ya barabara na simu ikiwa sikioni kwake.
"Ooh! Nasikia pia ulikanyaga-kanyaga kibanio changu. Zawadi nzuri kabisa kutoka Malyasia. Nimemletea anko wako lakini umekiharibu. Ila hamna tatizo, bali tatizo litakuwepo kama pale chini ulipokikanyagia kitabaki palepale. Najua kipo palepale, embu nenda kakiangalie." Mubah akatoka mbio tena na kuingia tena nyumbani kwake. Hapo alichokishuhudia, hakika hakuwahi kukifikiria katika kichwa chake.  Miili minne, akiwepo na yule mtoto ambaye walimfanya kama mjomba wa Muba ilikuwa imelala kifudifudi kwenye viti walivyokalia huku moshi mdogo ukiwatoka midomoni mwao. Nyuso zao zilijikunyata na kuwa kama za wazee wa miaka mia moja. Damu ilikaushwa katika miili yao kwa kutumia sumu kali inayosambaa kwa hewa.
Mubah alipoangalia sehemu alipokanyagia kile kibanio, alikuta kuna majivu machache ambayo yalitokana na kile kibanio kuungua.

USIKOSE SEHEMU YA SITA.. PAPA HAPA SIMULIZI MIX ENTERTAINMENT

0 comments:

Post a Comment