Thursday, July 6, 2017


NIENDE WAPI?‘’Dunia imenichukia’’
 IMELETWA KWAKO NA SIMULIZI MIX ENTERTAINMENT                    
MWANDISHI ZUBERY RAZUUR MAVUGO.

SEHEMU YA SITA.

ILIPOISHIA:
   
Siku iliyofuata, mtoto Maduhu akiwa kama mmiliki halali wa nyumba ile aliyoachiwa na wazazi wake. Hakuhitaji ushauri kutoka kwa yeyote aliyemzidi umri. Alitangaza mnada wa nyumba ile ambayo nd’o urithi wa pekee alioachiwa na wazazi wake. Kipindi cha nyuma baba Maduhu alipopata kiasi fulani cha pesa, aliamua kununua kiwanja na kujenga nyumba ile kwa ajili ya yeye na familia yake waweze kujistiri lakini leo hii mwanae shida zimemjaa na kuona njia pekee ya kutatua matatizo yake ni kuuza nyumba. Mshauri mkuu akiwa ni tumbo lake.

 ENDELEA...  Mnada ulikuwa mnada, watu wakanadika. Madau mbalimbali yakapandiliwa kutokana  na kwamba kiwanja kile kilikuwa kikubwa na licha ya ukubwa wake vilevile kilikuwa eneo zuri la mjini huku sehemu ile ikiwa njema kwa biashara.

     ‘’ Haya, huyu amesema milioni moja na laki tano... Wapi mwingine?’’ wakatokea wengi tu. Hapo dalali akaendelea kupandisha dau huku moyoni mwa Maduhu akifurahi na kuuambia kimoyomoyo umasikini kwa heri. Alijiwazia mwenyewe endapo angepata pesa hizo basi tatizo la chakula lingemwisha na milele asingehangaika kabisa, huku mawazo yake yakiwa ni kutafuta biashara ya aina yoyote ile iliaweze kuifanya itakayompelekea asiwe na matatizo. Ngawa alikuwa mdogo lakini alitambua mengi, ni wazi kabisa, baba yao alikuwa ni mtu mwenye mitazamo chanya na aliwajenga watoto wake katika misingi ya utafutaji ingawa walikuwa bado wadogo.

      Wenye malengo na kununua kiwanja kile kilichokuwa na nyumba mbovu waliendelea kupanda madau yao. Hakuna aliyekubali kuzidiwa dau hata kidogo, wakifikiria ni jinsi gani kiwanja kile kinaweza kuwaingizia fedha nyingi sana endapo wakijenga na kuanzisha biashara zao eneo lile. Hapo dalali akafika kwenye milioni tano na nusu.

            ‘’... Tano na nusu mara ya pili, nani anapanda dau? Tano na nusu mara ya tatu? Nne, tano? Sita? Saba? Nane? Tisa? Kumi?’’ Hakuna hata mmoja aliyeonekana kunyoosha mkono, isipokuwa mmoja tu. Dalali akamtangaza mtu yule kuwa yeye nd’o ameibuka kujinyakulia kiwanja kile.

Maduhu alifurahi sana, binafsi hakuwaza katika maisha yake kama ipo siku angeweza kumiliki hata laki moja. Leo kupitia nyumba ya wazaz wake anasikia wazi kabisa kuwa, muda si mwingi atamiliki mamilioni. Alijiona tajiri ghafla. Kabla hata hajazitia mikononi pesa zile alimshukuru sana Mungu.

    ‘’ Ebwana eh! Mimi pesa zangu zipo nyumbani... Sasa sijui twedeni mkachukuwe moja kwa moja? ‘’

  ‘’Eh! Twende hata sasa?’’ Maduhu aliwahi.

  ‘’ Wewe Maduhu, tulia.. Huruhusiwi kuongea, muongeaji ni mimi hapa.’’ Dalali alisema kisha akaongeza, ‘’ Kwenda nyumbani kwako hatuwezi. Si jambo zuri kumchukuwa mwenye kiti wa kitongoji mpaka mtaa unaoishi wewe. Unachotakiwa ni wewe kuja hapahapa ama tutafute sehemu tulivu kwa ajili ya jambo hili.’’

 ‘’ Oh! Sawa, basi ondoeni mashaka... Kwakuwa mimi hiki kiwanja nimekipenda sana, lazma nirudi... Wacha nikafuate pesa kisha nakuja hapahapa.’’

 Wakakubaliana. Lakini jambo lile kwa Maduhu aliona ni kama Dalali msumbufu tu, iweje jambo la watu kupeana pesa lichukuwe hatua nyingi kiasi hicho? Lakini hakuwa na namna kwa vile tayari alishakubaliananae.

 Wakabaki wamemsubiri yule mteja wao.

     ***

‘’ Mke wako hawezi kufanyiwa uparesheni bila wewe kutoa hizo pesa... Halafu ni muda mchache umebaki, ukizidisha sana unaweza kumpoteza.’’

  ‘’ Dokta? Ina maana hakuna njia nyingine ya kumsaidia? Tafadhali naomba unisaidie nikiwa kama mwanaume mwenzako. Nampenda sana mke wangu dokta. Nisaidie, nimejitahidi sana lakini nimeishia kupata shilingi elfu themanini. Tafadhali naomba msaada wako, mie hayo mamilioni kwa sasa sina uwezo wa kuyapata dokta?’’

   ‘’ Kiukweli bwana Mashaka, hapo sina njia ya kukusaidia. Hakuna namna, wewe leta hicho kiasi cha pesa ulichoambiwa, ilkituyaokoe maisha ya mwanao hivi sasa.’’

   Hakuwa na jinsi bwana yule kwa jina la Mashaka. Ni siku kadhaa tangu afukuzwe kazi kutokana na tuhuma ya upoteaji wa pesa katika kitengo alichokuwa akikisimamia ndani ya kampuni moja alilokuwa akifanyia kazi.

Muda huo hakuwa pesa, kila alipojitahidi kutembea kwa watu wake wa karibu na wao ni kama walimtenga wala wasiwaze kunisaidia hata kidogo. Kila akifikiria ni kipi hata angeweza kuuza ambacho kipo mikononi mwake, aliishia kukosa, ni bora hapo nyuma wakati akiwa na nyumba yake kubwa yenye kila kitu, kipindi hicho akiitwa bosi, kila sehemu yeye na suti. Si hivi sasa baada ya nyumba yake ya haja kupigwa mnada na kampuni alilokuwa akifanyia kazi, huku magari yake yote mawili yakiuzwa kwa bei ya kawaida ilimradi kampuni iokoe pesa zake ilizopoteza kitendo kilichompelekea apoteze kabisa mwelekeo wa maisha yake binafsi, asijue nini afanye.

 Hivi sasa aliamua kutoka ndani ya hospitali ile kubwa ya Bugando, hospitali ambayo hapo awali alikuwa akiifuata huku akiwa na usafiri wa gari, lakini kwa sasa alikuwa yeye pamoja na miguu yake. Hakuhitaji hata kumtazama mkewe ambaye hali yake ilikuwa hairidhishi. Machozi yalimtoka kwa wingi mtu mzima yule, akifikiria ni jinsi gani angeweza kuzipata hizo milioni mbili kwa ajili ya kuyaokoa maisha ya mkewe.

 Akapanda usafiri wa daladala baada ya kugundua kumbe mfukoni alikuwa na shilingi mia nane. Daladala ilipofika mjini alishuka na kuendelea na safari yake asijue wapi anaelekea. Akiwa njiani aliamua kuingiza mikono yake ndani ya mifuko ya suruali, hapo akakumbwa na mshangao kidogo.

 ‘’ Ina maana sijalipia daladala? Mbona konda hakunidai?’’ Akajicheka na kuamini kweli hakuwa katika hali ya kawaida, huku akiwaza, ni vipi konda amemruhusu kuondoka bila kulipia wakati yeye awajuavyo makonda, hakuna konda wa namna hiyo.

    Akiwa maeneo fulani mara aliweza kuliona gari moja la haja likipaki. Kisha akateremka bwana mmoja aliyefuatiwa na mabwana wawili, mkononi bwana yule alikuwa ameshikilia mkoba. Hakuwajali, akatamani kuendelea na safari zake, akiwa katika hatua mara alisikia.

   ‘’ Ila hizi pesa ni chache sana kwa kiwanja kama kile, lakini wacha tukakinunue tu. Halafu yule mtoto anaonekana ana njaa sana.’’

  ‘’ Bila shaka kile kiwanja ni cha urithi... Sasa mtoto huyo pesa atapeleka wapi?’’

   ‘’ Atajua yeye mwenyewe maana sisi hatuwezi kujua.’’

 Maongezi ya mabwana wale watatu yaliendelea na kuyavutia masikio ya bwana Mashaka.

 Hapohapo kwa harakaharaka bwana Mashaka akajikuta akipata wazo fulani ambalo liliikimbilia akili yake.

  ‘’ Milioni tano na nusu? Mungu wangu! Yaani mimi nina hangaikia milioni tatu. Ha! Tena mtoto mdogo? Hebu ngoja niwafuatilie.’’ Aliongea taratibu sana kiasi cha kujisikia yeye mwenyewe, kisha akaanza kuwafuata mabwana wale.

 Walifika kwenye kiwanja kimoja kikubwa ambacho kilikuwa na nyumba ndogo isiyotamanisha. Nje ya nyumba ile macho ya bwana Mashaka yaliweza kuwashuhudia watu wa tatu wengine huku mmoja kati ya watatu wale akiwa ni mtoto mdogo.

  Hakuwa mjinga kiasi cha kutojua kamba; mtoto yule kama ni muhusika basi wale wengine mmoja kati yao angekuwa bwana aliyemtafutia wateja huku mwingie akiwa kiongozi wa eneo lile. Mabwana wale watatu wakaingia ndani ya nyumba ile yeye akiwa nje huku hatua moja baada ya nyingine akiisoma.

  Eh! Mungu wagu, nadhani unayatambua matatizo yangu tena kuliko hata mimi. Nakuomba nisaidie hizi pesa zote ziingie mikononi mwangu. Tazama, endapo nitazikosa bila shaka mke wangu atapoteza maisha nakuomba mwenyezi Mungu naomba unihurumie mimi. Najua pengine hii ni njia ya wewe kuniokoa hivyo naomba pia unisimamie. Bwana Mashaka aliongea maneno yale huku akiwa amejibanza sehemu, akifuatilia kila kilichokuwa kikiendelea. Mate yakitamani kumtoka, moyo ukimwenda mbio, hakuna alichokuwa akikifikiria zaidi ya kuokoa maisha ya mke wake.

          ITAENDELEA.
KWENDA SEHEMU YA SABA BOFYA HAPA>> SEHEMU YA SABA

0 comments:

Post a Comment