Friday, July 7, 2017


NIENDE WAPI?‘’ Dunia imenichukia’’
IMELETWA KWAKO NA SIMULIZI MIX ENTERTAINMENT                     
MWANDISHI: ZUBERY RAZUUR MAVUGO.

SEHEMU YA SABA.

ILIPOISHIA:
      Eh! Mungu wagu, nadhani unayatambua matatizo yangu tena kuliko hata mimi. Nakuomba nisaidie hizi pesa zote ziingie mikononi mwangu. Tazama, endapo nitazikosa bila shaka mke wangu atapoteza maisha nakuomba mwenyezi Mungu naomba unihurumie mimi. Najua pengine hii ni njia ya wewe kuniokoa hivyo naomba pia unisimamie. Bwana Mashaka aliongea maneno yale huku akiwa amejibanza sehemu, akifuatilia kila kilichokuwa kikiendelea. Mate yakitamani kumtoka, moyo ukimwenda mbio, hakuna alichokuwa akikifikiria zaidi ya kuokoa maisha ya mke wake.

   ENDELEA... Sehemu ile alikaa kwa muda mrefu pasina kujua nini ambachokilikuwa kikiendelea ndani. Nani kwanini watu wale walichelewa kutoka namna hiyo? ingawa alikuwa pia na mashaka kama jina lake lakini alijipa imani lazma mambo yangemalizika muda si mwingi. Akabaki ametulia hivyohivyo huku macho yake yakiendelea kufanya uchunguzi.

      ***
  ‘’ Sasa inabidi hapa usaini kwa ajili ya uthibitisho kuwa umeuza hiki kiwanja.’’

  ‘’ Ah! Wazee.. Mbona siioni haja ya mimi kusaini? Kwakuwa tumeshakubaliana, nisingependelea tusainishane... ama hatuaminiani?’’

   ‘’ Hahahhaha.. Maduhu, kukwambia usaini haina maana kwamba huaminiki...’’

   ‘’ Kumbe maada yake nini dalali? Mnadhani hiki kiwanja sio urithi wa baba yangu? Ama nini?’’

  ‘’ Hii maana yake ni uthibitisho kuwa kiwanja umeuza kiuhalali. Haya maandishi ni msaada kwako na kwa mnunuzi hivyo kama kumsaidia, inabidi uweke sahihi yako hapa.’’

   ‘’ Haka katoto bwana, mbona maneno mengi mdomoni?’’ Mnunuaji wa eneo alisema.

‘’ Hawa ni watoto wa kisasa bwana.’’

 Kicheko cha furaha kikawatoka.

‘’ Hata hivyo, mimi naona kama mnanichanganya tu.’’

‘’ Kwanini?’’

‘’Katika maisha yangu bado sijabahatika kusoma, hivyo sijui hata hiyo saini inaandikwaje.’’

‘’ Ina maana kumbe ujanja wote huo hujui hata kusaini?’’

  ‘’ Ah! Wengine bado hatujabahatika kusoma, wenyewe simnaona umri wangu ulivo mdogo?’’

 ‘’ Haka katoto kana umri mdogo lakini kana mambo makubwa... Loh!’’


  Ha! Hapo ikabidi kazi iwe nyingine. Lakini hakukuwa na tatizo maana kwa mwenyekiti wa kitongoji hakukuwa mbali, kwakulitambua hilo akaomba atoke kidogo kwa ajili ya kumfuatia muhuli wa dole gumba mtoto yule iliaweze kutimiza haki yake.

 Wakati anatoka, Mashaka kidogo moyo wake ukapata afadhali maana alikuwa ameshaanza kuhisi huenda wasingetoka mida ile. Hapo pumzi nyingine zikamwijia, nguvu mpya za uvutaji subra zikamfikia. hata hivyo mwenyekiti yule hakuchukuwa muda sana tangu atoke, alirejea kwa mara nyingine na kumpatia mtoto yule haki yake. Hapo ndipo alipopatiwa na pesa zake zote, huku akimwachia dalali kiwango walichokuwa wamepangiana.

 Hakuwa na utani kwenye pesa hata kidogo, aliushikilia mkoba vyema kabisa tena bila masihara.

  ‘’ Vipi bwana naona una mashaka sana... Tukuitie maaskari wakusidikize?’’ Alitania mmoja kati ya wale watu waliyonunua kiwanja kile baada ya kumuona mtoto yule akiwa katika hali ya kutojiamini kutokana na kutowahi kushikilia pesa nyingi namna ile.

  ‘’ Hii haihitaji usaidizi wakubwa... Maaskari wataniomba kitu kidogo mimi sitaki kutoa chochote, niacheni tu mwenyewe.’’ Mtoto Maduhu aliongea maneno yale yaliyowapelekea wanunuzi wa kiwanja kile waangue kicheko. Hata hivyo hawakukawia sana, waliamua kulifuata gari walilokujanalo na moja kwa moja wakapanda kisha wakaianza safari ya kwenda walipopajua wenyewe.

 Dalali alimuaga mtoto yule na yeye kuchukuwa hamsini zake huku mwenyekiti akiwa ni kama ameshachukuwa dakika kadhaa tangu afike nyumbani kwake.

  Hivi sasa mtoto Maduhu alikuwa peke yake. Akitembea kwa kujishtukia huku pesa zilizokuwa ndani ya mkoba akiwa kazikumbata juu ya kifua chake. Alipita njia isiyo na watu wengi akihofia kupita njia yenye msongamano wa watu iliasije kuibiwa bure. Mawazo yake yote yalidhani huenda katika safari alikuwa yeye peke yake, kumbe sivyo.

 Bwana Mashaka alikuwa akimfuata muda wote. Kila Maduhu alipoigeuza shingo yake, Mashaka nae alijigeuza na kujifanya yupo bize na jambo tofauti, kumbe malengo yake yote yalikuwa ni ule mkoba ambao aliamini akiupata tu, atakuwa amepata kila kitu na kuyaokoa maisha ya mkewe.

   Hata Maduhu alipopita kwenye njia iliyohifadhi kiuchochoro kidogo. Hapo ndipo bwana Mashaka nadhiri yake alipotamani kuitoa. Kile alichodhamiria kukifanya aliona ni muda muafaka sasa. Kwa usaidizi wa maneno ya wahenga yasemayo, ‘Chelewa chelewa utakuta mwana si wako’ alimfuata kwa nyuma na kumpiga kabali shingoni mtoto yule kitendo kilichompelekea ashindwe hata kupiga kelele akabaki akifurukuta, macho yakimtoka huku akimwona malaika mtoa roho kwa mbali akimtamani.

 Kwa haraka ileile, Mashaka aliuchukuwa mkoba ule uliyokuwa mikononi mwa mtoto yule bila huruma akamsukumia pembeni ambako kulikuwa na miiba kitendo kilichompelekea aiparamie miia ile. Hapo Mashaka akapotea bila hata kuonekana machoni mwa mtoto yule. Maumivu ya miiba yalimfanya mtoto yule alie kwa uchungu huku akiishikilia shingo yake na kujitahidi kumeza mate maana koromeo lilikuwa limemkauka. Akajiinua huku akapiga ukunga  akijaribu kumfukuza mtu ambaye hakujua hata ni wapi alipoelekea. Saa moja lilipita akitafuta, masaa mawili, matatu lakini hakuchoka, moyoni mwake alijipa imani huenda angemwona mwizi wake. Aliendelea kuhangaika kutafuta hatimae giza lilianza kuingia ndipo hapo alipogundua kuwa, pesa zake zimeibwa na hawezi kuzipata tena.

Hapo ndipo akili zikamtuma aelekee kituo cha polisi kwa ajili ya kutoa taarifa iliaweze kupatiwa msaada.

   Hata alipofika kituo cha polisi na kuelezea shida yake ni kama alikuwa amedhamiria kuwachekesha na mwishowe kuwakera maaskari waliyokuwa zamu usiku huo.

   ‘’ Mimi mwenyewe na ukubwa wangu sijawahi kushika milioni tano.. Ije wewe mtoto mdogo tena uliyevalia mavazi ya watoto wa mtaa ni.’’

  ‘’ Afande, naomba mnielewe... Pesa zangu nimeibiwa sina mbele wala nyuma.’’

  ‘’ Hivi wewe mtoto, unavuta bangi eh! Ama umeona hauna sehemu ya kulala giza limeingia sasa unakuja kutusumbua ilitukupe hifadhi ya kulala. Afande Masele hebu chukua huyu mtoto weka ndani mara moja kwa kosa la kuvuta bangi na kuja kuleta vurugu kituoni.’’ Mtoto Maduhu hakuna msaada aliyoupata zaidi ya kuchukuliwa na kuwekwa rumande.

 Ndani ya maisha yake hakuwahi kuwaza hata siku moja kuingia sero. Alikuwa akiishia kuzisikia simulizi na mateso wayapatayo wale ambao wamewahi kuingia ndani mule. Kila alipozisikia simulizi zile, alimuomba Mungu asijewahi  kuingia ndani mule hata siku moja. Leo hii amejikuta yupo tena kiurahisi haswa! Hakuwaza kama kuja kwake kuomba msaada kungempelekea kufanyiwa tkitendo kama kile.

 Wakati mwingine wale tudhaniao ni wema kwetu na kuwaamini kama misaada, waweza kuwa chanzo cha maumivu na majuto kwetu. Moyo wa mwanadamu haubadilishwi kwa kazi anayofanya ama mavazi anayovaa bali kwa mapito aliyopitia.

      ***

 Mashaka alikuwa katika hali ya kujilaumu sana. Alijiona ni mmoja kati ya watu waliyoshiriki dhambi kubwa kuliko zote ulimwenguni. Katika maisha yake yote, amelelewa chini ya misimamo ya kidini, hakuwahi kuwaza hata siku moja kuchukuwa cha mtu bila ridhaa yake wala kuiba cha mtu. Ni amri kumi za torati ambazo hakuhitaji hata siku moja awahi kuzivunja lakini shida pekee ndizo zilizompelekea huko.

 Muda huo alikuwa ndani ya chumba chake ambacho ndicho alichopanga baada ya kukosa mbele wala nyuma. Pesa zile alizomnyang’anya mtoto wa watu, aliendelea kuzitazama hukuakihisi laana yake ina mwandama. Roho ilikuwa ikimuuma sana, akifikiria ni kwanini amemuumiza kiasi kile mtoto wa watu? Na je, mtoto yule aliyeonekanawazi kabisa kuwa anashida za muhimu mpaka kufikia kuuza kiwanja, ni wapi alipo muda huo? Je, Mungu atamsamehe kwa jambo lile.

  Usiku mzima nafsi ya Mashaka ilikuwa katika Mashaka tu.

Hata hivyo, kila alipokumbuka umuhimu wa maisha ya mkewe, hofu yote ilimwondoka. Akijisemea, ‘ Mungu anisamehe, maana sijafanya vile kwa kupenda’ huku akiiombea siku mpya iweze kuingia na yeye aelekee moja kwa moja hospitali kwa ajili ya kupeleka pesa na mkewe aanze kufanyiwa uparesheni maana alikuwa katika hali mbaya sana. Alijing’ang’aniza kuutafuta usingizi, ingawa hofu lilimchukuwa na kuutwaa usingizi wote lakini baada ya muda pasina hata mwenyewe kujielewa alijikuta akisinzia.


             ITAENDELEA.
KWENDA SEHEMU YA NANE BOFYA HAPA=> SEHEMU YA NANE

0 comments:

Post a Comment