Friday, July 7, 2017


DUKA LA ROHO SEHEMU YA KUMI
IMELETWA KWAKO NA SIMULIZI MIX ENTERTAINMENT
MWANDISHI FRANK MASAI

ILIPOISHIA
"Lisa yupo hatarini bila yeye kujitambua. Mume wake si mtu kama anavyodhani, muda wowote anamgeuka. Huyo ndio sababu ya Lobo kujua njia nyingi za FISSA kwa sababu anamuwekea GPS kila anapojua zimetolewa. Nakwambia haya lakini usimwambie chochote kile. Atakuja kuju a ya kumaliza mambo haya." Malocha alimuelekeza Mubah mambo kadhaa, kisha kuanza kumpa siri za Lisa ambaye alikuwa anacheza na mwanaye anayesheherekea siku yake ya kuzaliwa.
"Kwa hiyo mume wa Lisa anashirikiana na Lobo."
 ENDELEA
"Hilo ndilo jibu." Malocha akamjibu kifupi na kumuacha Mubah bila swali na badala yake akatwaa simu yake na kubofya namba kadhaa ambazo alimpigia simu Lisa.
****
 Ukimya ulitawala ndani ya gari alilochukua Mubah kwenda Kivule yalipo makao mapya ya FISSA ndogo ikiongozwa na Malocha. Ukimya huo ni kwa sababu Lisa alichimba mkwara ambao Mubah alikubali yaishe kuliko kuzidi kuchongoa mdomo wake.
Baada ya dakika kadhaa, walikuwa wamekwishafika kwenye nyumba hiyo ambayo wanaitumia kama makazi yao.
"Heee! Malocha leo upo huku." Lisa akamuita mkuu wake jina ambalo walishazoeana kuitana shuleni.
"Leo nimekuja kuwatembelea aisee." Malocha akajibu huku anatabasamu.
"Mmmh! Haya karibu." Lisa aliongea kwa sauti ya furaha huku akisogea kwenye kochi lililo sebuleni pale walipofikia.
"Hey. Martina, hujambo mama." Malocha akamsalimia Martina mtoto wa Lisa.
"Sijambo shikamoo."
"Marahabaa. Mimi ni Anko Malocha."
"Shikamoo Anko Malocha."
"Leo sherehe yako ya kuzaliwa. Nikupe zawadi nisikupeee." Malocha alimuuliza kwa furaha Martina.
"Nipee Ankoo." Martina naye akajibu huku mikono yake akiipunga kama vile kaungua. Malocha akatabasamu baada ya kumuona mtoto mwenye furaha kiasi kile.
Akaenda chumba fulani kisha akatoka na baiskeli moja ya rangi ya pinki, rangi ambayo hakuna watoto wa kike wasiyoipenda.
"Asante Anko." Martina alimshukuru Malocha na kumkumbatia kwa nguvu.
"Haya Martina. Nenda na yule pale mkaendeshe baiskeli huko." Malocha alimkabidhi Martina kwa jamaa mmoja ambaye alimchukua Martina na kumpeleka uwani mwa nyumba ile walipoanza kufurahia zawadi hiyo.
"Okay Lisa. Nimekuita hapa kukwambia kuwa FISSA tumefukuzwa kazi lakini tutarudi baada ya mambo fulani kukamilika. FISSA sasa hivi wameingia watu wapya lakini ni watu ambao kwangu mimi siwapi sana nafasi." Malocha akaweka tuo kabla ya kuzidi kutiririka.  "Sasa kwa kuanzia, tuanze na kazi ya kuutafuta ukweli kuhusu Lobo. Ila kwanza nataka kusikia kama upo tayari kufanya kazi na sisi." Malocha akatupa swali kabla hajaendelea na mengine.
"Nimezaliwa kufanya hayo. Siwezi kukataa na wakati huyo ndiye mimi." Lisa akajibu kwa kujiamini na Malocha akamchukua mwanadada huyu jasiri na kwenda naye kwenye chumba maalumu kwa ajili ya upelelezi. Wakati huo Mubah alikuwa kimya akiwafuata wafanyakazi wenzake kwa nyuma.
"Kazi yetu inaanzia hapa." Malocha akamuonesha gari ambalo waliling'amua namba zake.  Maelezo kadhaa yakaanza baada ya kumuonesha gari lile. Hiyo yote ni katika kumuelekeza Lisa ili aelewe nini sababu ya kuoneshwa picha hiyo.
"Sasa tumekwisha fatilia gari hili ni la nani na ninataka wewe na Mubah muongozane hadi kwa huyu bwana kisha mumuhoji maswali kadhaa. Kama hatojibu, basi tumieni mbinu za kumchukua na kumleta huku. Atajibu tu." Malocha akamaliza maongezi yale na kuwatazama watu wale.
"Hamna tatizo. Ila naomba mkae na Martina vizuri." Lisa akatoa ombi na.kuchukua dhana kadhaa kwa ajili ya kujilinda na kujijulisha (vitambulisho). Baada ya hapo akatoka nje na kuwaacha Mubah na Malocha wakiwa na opareta wao wakijadiliana.
"Mkuu. Wakati nazimia nilikwambia nimemuona mtu kwenye hii gari. Mtu huyo ni Gunner, mume wa Lisa. Kitu kilichonifanya nijue ni kibanio cha Martina ambacho ni sawa na kile ambacho kilimwaga sumu kule nyumbani. Na mbaya zaidi, huyu mtoto anafundishwa ujasusi na baba yake." Mubah akatoa taarifa kadha wa kadha hadi pale aliporidhika ndipo alipoamua kutoka nje akiongozana na Malocha.
"Hicho kibanio lazima kibaki ili nacho tujue ni wapi kimetoka." Malocha aliongea huku wakiendelea kwenda sehemu nyingine.
"Sawa mkuu. Ngoja sisi twende." Mubah alikubali wakati alipofika sebuleni na kumuona Lisa akiwa anawasubiri.
"Umemuaga kijana wetu." Malocha alimuiliza Lisa kama kamuaga Martina.
"Ndio. Naona hana tatizo. Yupo na furaha." Lisa akajibu huku akinyanyuka ambapo alitoka nje na kukwea gari ambalo wameandaliwa kwa ajili ya kwenda walipopanga. **** Majira ya saa moja jioni, Mubah, Lisa wakiwa na dereva wao, walifika eneo la Sinza na moja kwa moja wakaenda nyumba ambayo walipata maelezo kuwa mtuhumiwa wao anapatikana. Lakini cha kushangaza walipofika, walikuta watu wamefurika na vilio vikisikika huku na kule.
Walisogea na kuuliza kuna nini, wakajibiwa kuwa Mzee Mofo, ambaye ndiye walimfuata amefariki dunia kwa kuchinjwa kama kuku.
Ilikuwa ni hadithi ya kusikitisha kwenye kila kichwa cha aliyeisikia, lakini hakuna ambaye alikuwa tayari kuingilia hayo maswala kwa kuwashuku watu fulani.

"Lisa tunafanyaje sasa. Doa limeshaingia kwenye nguo nyeupe kama uonavyo." Mubah alimuuliza Lisa baada ya kufuata watu kadhaa na watu hao kutotoa ushirikiano wowote katika kujibu.
"Mambo magumu hapa Mubah. Ila tujitahidi tuonane na mke wake kabla hawajaenda mazikoni hiyo kesho." Lisa alishauri huku macho yakiwa yametua mbele ya mwanamke mmoja, mnene kiasi na mwenye weupe wa asili.  Alikuwa katika majonzi mazito na baadhi ya wanawake wenzake walikuwa pembeni yake wakimpooza kwa kila neno zuri.
Mara kwa mara alijigonga kifua na kuwa mtu wa kulalamika kwa lugha ya Kidigo.
"Sawa sawa. Yaonekana kuna jambo analalamika kwa sababu ya kifo cha mumewe. Ikibidi tumtoe pale sasa hivi tukamuhoji pembeni." Mubah alishauri kitu ambacho Lisa hakukawia kukifanya. Akasonga hadi pale ambapo yule mwanamke anapolia, na kisha kwa chati akamuomba watoke eneo lile mara moja wakazungumze.
Ilikuwa ngumu kwa mwanadada yule kukubali, lakini baada ya Lisa kujitambulisha vema, hatimaye mwanamke yule alikubali na kwenda naye katika chumba ambacho aliona ni sawa kwa kumpasha yote yaliyojiri.
"Sijui dada yangu. Roho inaniuma sana kumpoteza mume wangu. Ila yote hiyo ni kwa sababu ya upinzani wa kibiashara tu. Wameniulia mume wangu ofisini kwake, na kisha kwenye ukuta ule wameandika Duka La Roho." Ni maneno ya yule mwanamke akijaribu kuelezea kilichokuwa kinaendelea mbele ya Lisa, wakati huo Mubah alikuwa nje.
"Ofisi yake ipo wapi."
"Zipo Ukonga, Madafu."
"Okay. Ngoja twende huko tukaangalie taarifa yoyote. Naomba funguo za huko na kibali pia." Lisa aliongea na yule dada, kisha akamuacha atafute alichokihitaji.  Baada ya sekunde kadhaa, mke wa Mofo alikuwa amekamata funguo za ofisi zile za akiba na karatasi moja ambayo itasimama kama kibali.
Lisa akapokea vitu hivyo na kisha akataka kutoka mle ndani. Lakini ni kama Mke wa Mofo alikuwa kasahau jambo, akamuita huku akiwa na uoga mkubwa machoni pake.
"Dada. Maisha yangu pia yapo matatani kwa sababu ya mume wangu. Roho yangu pia ipo dukani. Njia ya kuinunua ni kutosema ukweli juu ya hili jambo. Lakini siwezi nikakaa na siri hii kwa sababu tayari mume wangu si naye tena. Naomba nikwambie wewe." Mke wa Mofo alikuwa akiangalia huku na huko wakati akitamka haya.
"Eheee! Niambie dada yangu." Lisa akasogea karibu na kumshika mkono na kumkalisha kwenye kitanda cha chumba kile.
"Mume wangu alikuwa anauza madawa ya kulevya na ni mshirika mkubwa wa makundi haya makubwa ya kuuza madawa. Watu kama Mafia, Yakuza nakadhalika, alishirikiana nao sana. Baada ya kuona kapata mafanikio, akaomba kujitoa kundini ili aendeshe maisha yake kiuhalali. Kitendo hicho kilimpa machaguo mawili. Kama anataka kujitoa basi auze roho yake au anunue. Yaani angetaka kununua roho yake, akubali kufirisiwa. Angetaka kuuza, basi afe lakini mali zitabaki chini ya familia yako. Wakampa siku mbili ya kununua au kuuza.
Mume wangu akadhani ni utani na hakuna ambaye ataweza kumuua. Akajidhatiti na kuweka walinzi nyumbani na popote alipokuwapo. Siku ya pili inatimia tu! Mume wangu akauawa na maiti kukutwa ofisini huku mwili umekaa kwenye kochi na kichwa kimewekwa juu ya meza." Mke wa Mofo alimaliza maelezo kadhaa anayoyajua.
"Hiyo kampuni ni yake kweli?" Lisa akatupa swali lingine na kumfanya yule dada kuzidi kuwa na mashaka. Ila kwa kuwa aliyavulia maji nguo, basi kuyaoga ni njia inayofuata.
"Si ya kwake. Na ndio ofisi kubwa ya kusambaza madawa nchini Tanzania." Akajibu dada wa watu.
"Sasa ipo chini ya nani?" Mke wa Mofo akaangalia tena pande kadha wa kadha ijapokuwa chumba kile walikuwamo wawili tu. Akasogea karibu zaidi kwa Lisa na kwa sauti ya chini akaanza kujibu.

"Ipo chini ya tajiri mmoja Mkam......" Kimya kikamkumba dada yule. Hakumaliza sentensi yake. Lisa alipomuangalia mwanamke mwenzake, alimshuhudia akidondoka kitandani kama mzigo huku damu zikimvuja kichwani palipokuwa pana tobo la risasi. Ukuta nao ulikuwa umechafuka kwa damu hizo.

ITAENDELEA

KWENDA SEHEMU YA KUMI NA MOJA BOFYA HAPA=>SEHEMU YA KUMI NA MOJA 

0 comments:

Post a Comment