Friday, July 7, 2017

NIENDE WAPI?‘’Dunia imenichukia’’
IMELETWA KWAKO NA SIMULIZI MIX ENTERTAINMENT                       
MWANDISHI ZUBERY RAZUUR MAVUGO.

  SEHEMU YA KUMI.

ILIPOISHIA:
   Uvumilivu ulimshinda mtoto yule, yaani hajaiba cha mtu halafu anaumizwa namna ile kwanini hasa? Hapo akayachukuwa macho yake mawili na kuyaangazisha chini, kisha akaanza kuyatembeza huku na kule mpaka hapo alipofanikiwa kuliona jiwe lililokuwa limeshangaashangaa mchangani, tabasamu lakujilazimisha likamtoka. Akalifuata jiwe lile kwa mwendo wa upesi, hata alipoliokota kitendo bila hata kuuliza wala kuomba ushauri kwa yeyote alilivurumisha jiwe lile hadi alipokuwa mwanamke yule.

   ENDELEA..   ‘’ Yalaa! Mtumee! Nakufaa... Jamani nakufaa...!’’ Mwanamke aliangua kilio cha namna ile baada ya jiwe kutua vyema mkabala na jicho lake kitendo kilichompelekea apate maumivu ya haja. Hapo yule mtoto amani ikamwingia, kitendo bila kuuliza akaianza safari ya kutimka eneo lile na kukatiza wala asionekane na asijulikane wapi alielekea.

       ‘’ Wewe... Wewe kaka, simama tafadhali.’’ Binti ambaye muda wote alikuwa akimfuatilia, hakuhitaji kumwachia hata kidogo, safari hii alipoona mbio za mtoto yule zimemshinda akaamua kumwita. Mtoto Maduhu hakuhitaji hata kugeuka nyuma, nd’o kwanza aliongeza mwendo wa kukimbia, mpaka hapo alipoisoma sauti ile vyema ndipo alipogeuka na kumgundua binti yule. Akarejea kumfuata.

‘’ Hivi wewe... Unanitafuta nini hasa?’’ Alisema.

  ‘’ Usiniulize maswali ya kipuuzi,’’ Binti yule mwenye umri wa miaka kumi na mmoja alisema maneno yale. Wakati huohuo hata bila kuuliza swali, aliuvua mtandio wake aliyokuwa kajifunga; mtandio ambao aliununua kufuatia malipo ya mwezi wa awali aliyofanyia kazi. Akauchana bila kuuhurumia na kuuchukuwa mkono wa Maduhu ambao ulikuwa na kidonda, akaustiri mkono ule kwa kuufunga na mtandio ule huku yeye kichwani akibakiza kitambaa kidogo pekee.

 ‘’ Kwanini umefanya hivi?’’ Maduhu alihoji huku akiendelea kumwangalia binti yule kwa mshangao.

   ‘’ Kwasababu sipendi kumuona mtu akiwa katika hali kama hii’’

    ‘’ Lakini sijakuomba msaada.’’

     ‘’ Kwani hata mimi nimetaka kukusaidia?’’

     ‘’ Donda sila kwangu?’ kwanini likutie kiherehere’

     ‘’ Hata kama, ila mimi sipendi kutazamana na watu wenye vidonda kama wewe’’

      ‘’ Sawa, kwakuwa sikukuomba, sina haja ya kukushukuru ila siku moja nitakulipa gharama ya mtandio wako uliyoupoteza.’’

     ‘’ Nami naisubiri siku hiyo, andika deni katika maisha yako.’’

     ‘’ Nitakupatia wapi?’’

      ‘’ Sihitaji kutafutwa, kwanza wachamie niende zangu.’’

  Binti yule alipomaliza kuyanena yale, hapo akaianza safari ya kuondoka zake huku Maduhu akimshuhudia wala asijue amfuate ama aendelee kuwepo eneo lile. Maswali mengi kichwani yalimuijia, akijiuliza, huyo binti ana roho gani? Mbona ni yeye aliyeonesha msaada na si wengine. Ina maana binti yule anawazidi mioyo watu wengi ndani ya jiji hilo? Lakini asipate majibu.

 Aliamua kuendelea na safari yake huku akiwaza mambo yake binafsi kuliko kujishughulisha na jambo lile. Akiwa njiani kuelekea asipopajua, alipita kwenye dumu la uchafu wa genge na kukuta ukoko umemwagwa, hapo hata hakuuliza swali, akaukimbilia ukoko ule, hata alipoufikia alianza kuula kwa pupa, baada ya hapo tumbo lake lilikuwa limejaa kiasi kwamba alitamani asinzie tu na sikufanya chochote.

 Usingizi ulimchukuwa pembezoni mwa genge alilopatia mlo wake. Hapo akawa hajitambui tena ndani ya usingizi mzito huku akiufidishia na ule wa siku iliyopita maana hakulala zaidi ya kushambuliwa na mbu kituoni.

    ***

Siku zilizidi kuyoyoma, hatimae ile siku ambayo bwana Mashaka alikuwa akiisubiria kwa hamu iliwadia. Siku hiyo aliitwa na daktari kisha akaambiwa kuwa tayari mkewe anaendelea vizuri na ruhusa ingetoka sikuhiyohiyo. Hapo akajionea fahari haswa. Baada ya muda aliruhusiwa kwenda kumtazama mkewe, hakuamini kama mke wake alikuwa akipumua vyema na kuongea vizuri, alimshukuru sana mola wake.

  Hata pale daktari alipotoa ruhusa yake, wallifurahi wote wawili na moja kwa moja wakatafuta usafiri wa taxi na kuelekea nyumbani kwao.

Mashaka hakuwa ndani ya nyumba ambayo alikuwepo awali, nyumba isiyo tamanika, isiyo heshimika wala isiyolalika. Hivi sasa alikuwa ndani ya nyumba moja ya haja ambayo alikuwa tayari ameilipia kodi ya miezi sita; nyumba yenye umeme, na kila kitu cha kawaida.

  ‘’ Ha! Mume wangu? Upepatia wapi pesa za kupaga kwenye nyumba nzuri kama hii? Nakumbuka mara ya mwisho tulikuwa tukilala ndani ya kibanda tena chini... Vipi tena?’’ Mkewe alihoji.

  ‘’ Mke wangu, mwenyezi Mungu humpatia rizki amtakae bila hata kumuhesabia... Wakati ukiwa hospitali hakika kichwa changu kilivurugika sana. Nikalihisi kaburi langu likiniijia.’’

  ‘’ Sio wewe tu, hata mimi. Binafsi nilikuwa nimeshakata tamaa, sikuwa na imani tena wala sikuwaza kama wewe utaweza yaokoa tena maisha yangu... Nashukuru sana mume wangu.’’

  ‘’ Hata hivyo, niliamua kujivika ngozi ya chui ilikuhakikisha yote yanatimia.’’

   ‘’ Una maana gani katika maneno yako?’’

    ‘’ Sina maana yoyote ile mke wangu, hebu ingia chumbani kapumzike wachamie nitulie hapahapa sebuleni maana nimechoka hatari.’’

  Mashaka aliamua kujipumzisha sebuleni huku akitazama runinga, akiwa usingizini mara ndoto moja kali ilimwijia. Akaota anakimbizwa sana na mtu aliyeshikilia panga. Ingawa alijitahidi sana kukimbia, lakini kamba ya kiatu chake ilimponza baada ya kujifungua na kumtega mguuni kitendo kilichompelekea aweze kuanguka chini, hapo yule mtu mwenye panga akamfikia. Alipomtazama sura hakuwa mwingine bali ni yule mtoto kwa jina la Maduhu.

  ‘’ Unajua ninateseka kwa kiasi gani mpaka hivi sasa? Ina maana uliamua kuniibia pesa zangu na kumfaidisha mkeo huku ukifaharika kwa kupata mtaji pamoja na kodi ya nyumba eh! Sasa leo nakuua ili ukayahisi maumivu yangu huko kuzimu’’ Mtoto Maduhu baada ya kutamka maneno yale, hapo akalichukuwa panga na kuamua lizamisha mwilini mwa bwana Mashaka. Kitendo kile kiliweza kumfanya apige makelele. Hapo akashtuka ghafla huku bado ukelele ukimalizia kumtoka.

 ‘’ Nini tena mume wangu? Mbona unanishtua wakati nimejipumzikia chumbani?’’ Mkewe alihoji baada ya kutoka chumbani mwake mbiombio.

  ‘’ Ah! Hakuna kitu, ni ndoto tu.’’ Mashaka alijibu huku akiwa katika hali ya woga.

  ‘’ Ndoto? Mchana huu?’’ Mkewe alisaili.

  ‘’ Hata mimi ninashangaa...!’’

  ‘’ Mh! Haya nieleze umeota nini hicho kilichokufanya uwe katika hali hiyo na kupiga makelele hovyo.’’

   ‘’ Hakuna kitu mke wangu... Wala usijali.’’

 Hata hivyo Mashaka alimficha mkewe ndoto aliyoiota. Hapo akatoka nje na kwenda zake kwa ajili ya kulitafakari jambo lile kiundani na kuangalia kama lina ukweli ama ni ndoto tu.

   Akiwa katika tafakari mara alisikia simu yake ikiita.

‘’ Eh! Haloo... Ule mzigo tayari umeshafika, ni wewe tu tunayekusubiri mpaka hivi sasa.’’

 ‘’ Basi sawa nakuja muda simrefu.’’

  ‘’ Sawa usichelewe.’’

Mashaka baada ya kupokea simu ile akajikuta mawazo yote yakimwisha na moja kwa moja akamfuata mkewe kisha akamwachia kiasi cha shilingi elfu kumi. ‘’ Nunua chochote ule, bado sijanunua jiko na vyombo vya kupikia... Kuna sehemu naelekea nitaporejea tutaongea zaidi.’’

 Alipoagana na mkewe akatoka, na moja kwa moja akaelekea kwenye kituo cha daladala, hata alipofika alipanda magari yaelekeayo mjini. Yalimtua na yeye akaanza safari ya kulifuata soko kuu. Alipofika ndani ya soko hilo alielekea upande wa wauzaji wa kuku na moja kwa moja akawafuata mabwana watatu waliyokuwa wamesimama pembeni kidogo, akawasalimu na wao  wakamwitika kama kwamba wanafahamiananaye kisha, wakamlaumu kwa kuchelewa, alizikubali lawama zile na mazungumzo yakaanza.

    ITAENDELEA.

KWENDA SEHEMU YA KUMI NA MOJA BOFYA HAPA=> SEHEMU YA KUMI NA MOJA

0 comments:

Post a Comment