Friday, July 7, 2017


NIENDEWAPI? ‘’ Dunia inanichukia’’
IMELETWA KWAKO NA SIMULIZI MIX ENTERTAINMENT                     
MWANDISHI: ZUBERY RAZUUR MAVUGO.

SEHEMU YA KUMI NA MBILI.

ILIPOISHIA:
     Baada ya maneno hayo machache akatoka ndani ya duka lile la simu na kuelekea kwa jamaa yake mmoja mrusha miziki. Wakasalimiana kwa salamu zao kisha akamwelezea kuhusu simu ile na kumwambia endapo atamtoa shilingi elfu ishirini tu basi kila kitu watakuwa wamemaliza. Rafiki yake yule hakutaka hata kuuheshimu uzuri wa simu ile, hapo badala aombe, yeye akashusha bei na kung’ang’ana apewe kwa shilingi elfu kumi simu ile ya laki na nusu.

ENDELEA...  ‘’ Ah! Ndinga, ina maana hata huoni kitu kilivyo kikali hiki? Kiukweli kwa kumi sifanyi... Yaani dude la laki na nusu wewe ulichukuwe kwa kumi?’’

       ‘’ Basi kama hutaki acha... Ila kumbuka mimi nakulinda kishkaji, sawa dude la pei ndefu ila kama kutatokea chochote unadhani wa kwanza kukamatwa ni nani? Si mimi mnunuzi.’’

       ‘’ Kwahiyo ndinga langu kumbe nimeyaweka maisha yangu lehani kwa ajili ya elfu kumi eh!’’

‘’ We kimavi nini? Sasa pigo gani unaniletea... Kama hutaki sepa, sio unaanza majungu. Mbona hata mimi ninayaweka maisha yangu hatarini kwakununua kitu cha wizi. Wakija ulowaibia na kunikamata? Hebu tembea, tafuta washkaji wengine ndinga.’’

  Hata hivyo wawili wale kuzungumza mazungumzo yaliyojaza lugha za kihuni, walifikia muafaka baada ya Maduhu kuikubali pesa ile kwani alikuwa na njaa sana.

  Hata alipopatiwa ile pesa, alielekea kwenye moja kati ya magenge yaliyokaribunae hapo akaingia na kuagiza chakula alichokuwa akihitaji, baada ya hapo alikula na kuanza elekea sehemu ambayo huutafuta usingizi wake kwani usiku ulikuwa umeshafika muda.

 Alitembea hadi kwenye nyumba moja isiyopendeza; nyumba ambayo ukiitazama kwa nje basi unauwezo wa kuviona vilivyo hifadhiwa ndani bila wasiwasi wa aina yoyote. Aliingia na kutandika sandarusi kisha akaanza kuutafuta usingizi wake.

               ***

  Siku hiyo bwana Mashaka alichelewa kidogo kuamka, hiyo ni kutokana na usiku wa jana kuusherehekea akiwa na mke wake, wakikumbushana mengi ya kimiili ambayo walikuwa wameyakosa kwa kitambo. Hata alipoamka bado alikuwa juu ya kitanda huku akiupa sifa mbalimbali usiku wa jana kimoyomoyo. Baada ya kukaa sana juu ya kitanda hivi sasa aliamua kuamka na kuelekea moja kwa moja msalani, alipotoka huko alifanya hatua zote za kuusafisha mwili wake.Wakati akifanya yote hayo, tayari mkewe alikua kisha amka zamani wakati huo alikuwa akifanya kazi nyingine za asubuhi, bila kusahau upishi kwani jiko kwa ajili ya kupikia aliletewa siku iliyopita na mume wake pindi aliporudi kutoka mihangaikoni.

   Baada ya Mashaka kumaliza vyote alivyokuwa akivifanya, tayari alikuta mkewe ameshamaliza upishi wa chai. Akakaribishwa chai na kunywa, baada ya hapo aliaga. Moja kwa moja akaianza safari ya kuelekea mjini ambako ndiko biashara zake za uuzaji kuku alipozianzishia.

       Hata daladala ilipomtua, nje kidogo ya soko kuu baada ya kumaliza kulipia. Aliamua kuelekea moja kwa moja hadi ndani ya soko. Alipofika kazini alianza harakati zote na kufanya mambo yote yaliyohusiana na kazi yake.

          Wateja waliendelea kumiminika na kumfuata yeye kutokana na jinsi alivyojua kuwajali kwa kauli zilizo hifadhi maneno matamu kama sukari, kitendo kilichoanza kuwakera wenzie waliyokuwa karibunae wakifanyanae biashara moja. Kwakuwa yeye ni mzoefu wa biashara ile, aliligundua jambo hilo lakini hakutaka alijali maana alitambua mambo kama hayo huwa hayaepukiki hata kidogo.

     Saa tisa alasiri kiu kililisumbua koromeo lake ipaswavyo huku njaa ikiliadhibu tumbo lake kana kwamba alitoka nyumbani kwake bila kupata chai nzito kutoka kwa mkewe. Ilibidi avumilie kwani bado wateja alikuwanao lakini baada ya muda kidogo aliamua kutoka kwa ajili ya kuyatafuta magenge ya chakula ambayo yangeweza kumtatulia shida ya tumbo lake.

Alipofika magengeni alilifuata genge moja na kuagiza chakula. Wakati akiwa nje ananawa mara alijikuta akisisimka mwili wake mzima, ni baada ya kuitazama sura ambayo hakuwa ametarajia kuiona; haikuwa sura nyingine bali ni ya yuleyule mtoto aliyewahi kumkaba na kumpora pesa ambazo zilimfanya apate mtaji na kuyaokoa maisha ya mkewe. Ingawa alijua mtoto yule hakumuona siku ile lakini bado aliona haya. Ajabu mtoto yule nae alikuwa akionekana kulifuata genge hilo.

 ‘’ Hata hivyo hanijui.’’ Mashaka alisema kisha akaingia ndani ya genge na kukaa kisha akaanza kupata chakula alichokihitaji. Wakati akipata chakula, mtoto yule kwa jina la Maduhu nae aliingia na kuketi mkabala na sehemu aliyokuwa amekaa Mashaka. Amani ikamponyoka, akajikuta hali kwa raha kabisa, mpaka mtoto Maduhu anamaliza kupata chakula chake, bado Mashaka alikuwa hajakimaliza cha kwake.

  Maduhu alitoka ndani ya genge lile na kulipia kiasi cha pesa alichokuwa akidaiwa kisha akaianza safari ya kuondoka eneo lile. Hapo kidogo Mashaka akajikuta akipumua kwa amani.

  Wakati hata kabla Maduhu hajafika mbali kutoka eneo lile, mabwana wawili waliweza kumuona na kumtambua. Ni yeye aliyemuiba mmoja kati yao saa ya mkononi pindi alipotoka kuinunua siku mbili zilizopita. Hawakutaka kumchelewesha baada tu ya kumuona hapohapo wakampigia mwano.

  Mtumee!

 Wananchi weye hasira kali, wenye kuujua uchungu wakuibiwa, wale ambao walisha apa katika maisha yao watakuwa radhi kuhakikisha wanawaondoa wote wenye kuiba vya watu ndani ya dunia hii. Walimfuata kijana yule huku wakiwa wameshikilia vya kushikiliwa na visivyo vya kushikiliwa, huku wengine kutokana na hamu ya kupiga mwizi wakijikuta hata wakisahau kushikilia vifaa vyovyote, badala yake wakajikuta wakienda hivyohivyo na ngumi zao.

  Hata walipomfikia mtoto yule ambaye na yeye aliposikia neno ‘mwizi’ hakuuliza na kuanza kukimbia, hawakumtaka maelezo.

  Hakuna hata mmoja aliyeuhurumia umri wa mtoto yule mdogo, waliyompata walimpa kipigo cha haja; kipigo ambacho hupigwa mbwa asiye na kwao, mbwa mwenye kurandaranda mtaani kila muda. Ndani ya dakika moja tayari mtoto yule alikuwa chini huku damu zikimchuruzika maeneo mbalimbali ya mwili wake, akijililia tu, lakini hiyo isiwe sababu ya yeye kuachwa na watu wale wenye hasira kali.

Sauti zile ziliweza kupenya hadi ndani ya ngoma za masikio ya mlaji mmoja kwa jina la Mashaka, aliyekuwa gengeni akiendelea kukishughulikia chakula. Hakuzijali sauti zile kwani ndani ya jiji hilo kubwa ni jambo la kawaida, mtu ama watu kuibiwa na kukamata mwizi kisha kupiga hadi kuua endapo nafasi hiyo ikipatikana.

 Hata hivyo alimaliza chakula chake vyema na hivi sasa alilipa gengeni kisha akaanza kuondoka zake. Alipolifikia eneo la tukio, hakutamani walau kwenda kumtazama mwizi yule aliyekuwa akipigwa kwani endapo angeenda kwa ajili hiyo bila shaka nae angetaka kumpiga tu.

Chakushangaza. Moyo ulimtuma aende walau kumtazama mwizi yule ambaye alitarajiwa kuuacha uhai wake muda mfupi ujao kutokana na kipigo alichoendelea kukipata kutoka kwa raia.

Alipofika, alisukumana na mabwana waliyokuwa wamezunguka eneo lile kisha akafanikiwa kumwona mwizi yule. Kwa mara nyingine mwili mzima ulimsisimka, baada ya kumwona mtoto aliyekuwa amevalia mavazi kama yale ya yule aliyekula nae, tofauti ilikuwa ni kwamba; yule mtoto aliyekuwa naye gengeni yeye hakuwa na damu mwilini ila huyo aliye hapo chini huku akipata kipigo yeye alikuwa na damu nyingi mwilini mwake. Moyo wa kutamani kumsaidia mtoto yule ukamwijia maana aliamini hata kipigo anachokipata mtoto yule kilifaa akipate yeye kwani ndiye msababishaji wa maisha ya namna ile kwa mtoto yule.

    Akawaza mbinu gani aitumie ilikuwashawishi raia waweze kumwacha mtoto yule, akiwa katika hali ya kuumiza kichwa, ndipo hapo wazo kuu lilipoichukuwa akili yake.

   ‘’ Jamani polisi wanakuja, tukimbieni, tusije kamatwa.’’ Aliropoka, sauti yake ilisikika na hivi sasa raia walimsahau mwizi wao na kuanza kukimbia. Ndani ya sekunde kadhaa eneo lile lilibaki jeupe halina mtu isipokuwa Mashaka pekee. Hapo akawa amefanikisha adhma yake, akawaza nini afanye kwa mtoto huyo ambaye alikuwa amepigwa sana. Hakuona mtu yeyote aliyeonesha kumjali, hivyo akaamua kulisimamia jambo lile zima mwenyewe.


              ITAENDELEA.
KWENDA SEHEMU YA KUMI NA TATU BOFYA HAPA=>SEHEMU YA KUMI NA TATU

0 comments:

Post a Comment