Friday, July 7, 2017


NIENDE WAPI? ‘’Dunia imenichukia’’
IMELETWA KWAKO NA SIMULIZI MIX ENTERTAINMENT                    
MWANDISHI ZUBERY RAZUUR MAVUGO.

SEHEMU YA NANE. 

ILIPOISHIA:
    Hata hivyo, kila alipokumbuka umuhimu wa maisha ya mkewe, hofu yote ilimwondoka. Akijisemea, ‘ Mungu anisamehe, maana sijafanya vile kwa kupenda’ huku akiiombea siku mpya iweze kuingia na yeye aelekee moja kwa moja hospitali kwa ajili ya kupeleka pesa na mkewe aanze kufanyiwa uparesheni maana alikuwa katika hali mbaya sana. Alijing’ang’aniza kuutafuta usingizi, ingawa hofu lilimchukuwa na kuutwaa usingizi wote lakini baada ya muda pasina hata mwenyewe kujielewa alijikuta akisinzia.

   ENDELEA... Jua lilichomoza na kuurejesha ufahari wake katika dunia. Huyu na yule wakaonana kwa umakini huku likileta ofa yake ya vitamini ndani ya dunia. Kuchomoza kwa jua kulimpelekea bwana Mashaka atambuewazi kuwa tayari siku mpya ilikuwa imewadia. Akanyanyuka kutoka juu ya godoro lake dhoofu, lisilo na kitanda, lakutandika ardhini. Kisha akalifuata jagi moja ambalo kwa ndani lilikuwa limehifadhi maji. Mswaki uliyotumika mpaka ukasema naomba usinitumie tena, nd’o huo aliyoufuata tena bila haya, badala auwekee dawa yeye alichukuwa chumvi na kupakaa juu ya mswaki ule kisha akaelekea kujisafisha.

   Muda kidogo alirejea ndani mwake, jicho la kwanza alilitupia kwenye mkoba uliyohifadhi pesa. Akakenua meno yake baada yakuuona ukiwa juu ya godoro. Akaendelea na mambo yake. Hata alipomaliza kila kitu, hapo aliuchukuwa mkoba ule kisha akaufunua kwa ndani na kukutana na pesa za kumwaga. Hakuwa na muda wa kuzihesabu bali alichojali ni kuhesabu pesa alizotakiwa kuzipeleka hospitali kwa ajili ya kuyaokoa maisha ya mkewe.

   Alipopata fungu alilolihitaji, aliamua kuuficha mkoba ule ndani ya mfuko wa rambo ambao alikuwa akiutumia kwa ajili ya kuhifadhia nguo zake, kisha akaondoka huku pesa zile akiwa amezifunga kwenye kitambaa alichokikuta ndani mwake.

Usafiri wa daladala ni kama aliuona utamchelewesha, ikabidi aite taksi.

‘’ Nipeleke Bugado hospitali... Fasta.’’ Alisema.

 Sekunde kadhaa mbele dereva aliwasha gari na kuianza safari ya kuelekea Bugando. Hawakuchukuwa muda sana, tayari walikuwa wameshafika, akashuka na kumlipa dereva kiasi cha pesa alichohitaji kisha kwa mwendo wa kuwahi akaichukuwa miguu yake hadi ndani ya hospitali. Humo tena alichukuwa muda hadi kuonana na daktari, hata alipoonananae aliongeanae kwa nyodo na maringo. Mwisho wa siku suala zima la ukoaji wa maisha ya mkewe lilianza bila tabu wala wasiwasi.

   Madaktari bingwa wa upasuaji waliihifadhi miili yao ndani ya mavazi maalumu kwenye  chumba cha upasuaji. Mwili wa mke wa Mashaka ukiwa juu ya kitanda maalumu, huku madaktari wakifanya mambo ya kutisha juu ya mwili wake na wala wasihofu chochote kile.

        ***

  Mpaka majira ya saa tano, mtoto Maduhu bado alikuwa ndani kafungiwa. Akiwa katika hali ya mchoko haswa. Hakutaka kuamini kama ni yeye aliyelala usiku wa jana ndani mule. Hakutaka kujikumbusha mateso aliyoyapata kulala katika nyumba ndogo iliyojaa kila aina ya kinyaa, kuachilia mbali yeye kujikunyata juu ya mikojo mpaka asubuhi, vilevile alishindwa kuwasahau mbu wenye roho mbaya kuliko hata magaidi. Mbu wenye sifa za kuwinda zaidi hata ya simba wa nyikani. mbu wale nd’o waliyomfanya usiku wa jana aufananishe na usiku wa kwanza wa jahanamu yake.

   Hata hivyo bado alikuwa katika mawazo makali sana, ni vipi amewekwa rumande ilhali hana kosa ama ndivyo sheria za nchi yake zilivyo? Alitamani aonane na mtaalamu wa maswala ya sheria iliangalau aweze kukiomba hicho kifungu kinachoruhusu mambo hayo, lakini tamaa zake zilikuwa ni sawa na bure.

      Muda huohuo nd’o muda aliyomuona afande mmoja akichungulia ndani ya chumba kile kupitia uwazi mdogo; afande yule hakuongea chochote zaidi ya kufungua mlango na kumtazama Maduhu kwa jicho la hasira.

   ‘’ Shikamoo...’’ Maduhu kama ilivyo kawaida yake ya kuheshimu wanaomzidi umri alisalimu. Afande yule alimsikia lakini hakumwitika, Maduhu akabaki amemtumbulia macho afande yule.

   ‘’ Mbona unaniangalia utadhani unataka kunimeza..’’ Afande alisema kisha akaongeza, ‘’ Usinitazame namna hiyo mimi... Alaaa! ’’ huku rungu likitua mwilini mwa Maduhu.

   Ingawa aliyapata maumivu lakini hakulia, alibaki akijishika eneo aliloumia huku macho yake safari hii akiyaweka chini.

   Afande yule akamchukuwa na kwenda kumpatia mavazi yake pamoja na viatu alivyokujanavyo siku ya jana.

‘’ Leo tena unakaribishwa uje kulala kama ukikosa pakulala.’’ Alisema hivyo na kuwafanya maafande wenzie wabaki wakikenua meno yao . Wakamsifia na yeye kichwa chake kikakua. Hapo Maduhu akaruhusiwa kuondoka.

   ***

 Hata alipokuwa akielekea hakuwa akipajua, njaa iliendelea kulisumbua tumbo lake pia. Hakujua ni wapi angeweza kupatia chakula. Aliona sehemu pekee ni yeye kujipitisha katika maeneo mbalimbali yenye magenge.

  ‘’ Eeeeeh! Wewe, hebu toka hapa.’’ Mama mmoja aliyekuwa akiuza genge, aliongea maneno hayo baada ya kumuona kijana yule.

  ‘’ Kwani nimekosea nini Mama... Mbona namimi ni binadamu kama wengine?” Alijibu huku akijitazama katika hali yamshangao.

   ‘’ Bado husikii? Binadamu?! Hivi nanyie machokoraa mnaubinadamu gani? Eh! Licha ya mimi kuwa mwema na kuwapatia ukoko bado mnaniibia mpaka pesa zangu... Tena toka. Sina huruma nanyie hata kidogo, panya mabaka ninyi.’’

  Ingawa hakupenda kuitwa chokoraa lakini hakuwa na jinsi, alikubaliana na jina lile. Taratibu akaanza kuondoka huku mama yule akitoa maneno ya kashfa pasina kujua ni mateso gani kijana yule anayapitia na ni kiasi gani utumbo wake unahitaji chakula.

 Katika pitapita zake kama mpita njia mwenye ndoto za kulikomboa tumbo lake, aliweza kupita kwenye genge jingine, huko akashuhudia kitu cha ajabu. Ati, wali na mfupa wa nyama vinawekwa katika mfuko wa kumwagia uchafu. Alimtazama mwanamke yule aliyeuweka wali ule kwa jicho la shukurani, kisha taratibu akaanza kulifuata fuko lile la kuhifadhia uchafu kama hataki.

  Akiwa njiani mara ghafla aliweza kushangaa, baada ya kumuona mbwa mmoja akiukimbilia mfuko ule huku ulimi wake ukiwa nje, udenda ukimtoka kwa fujo; mbwa yule ambaye hata mwili wake mzima ulikuwa umenyonyoka manyoya yake kutokana na kuyazoea maji ya moto aliyokuwa akimwagiwa kila mara, bado hakuwa amekata tamaa, ingawa pia alikuwa amejawa na madonda kutokana na kupigwa ovyo kitendo kilichompelekea aonekane dhohofulhali na mwenye magonjwa ya kila aina. Aliufuata mfuko ule.

 Mtoto mwenye njaa kali hakuhitaji kukubali jambo lile litokee hata kidogo. Ni vipi angeweza kulinusuru tumbo lake dhidi ya njaa kali aliyokuwanayo? Akaona njia pekee ni yeye kushindana na mbwa yule hadi kukiwahi chakula.

Hapo akakaza mwendo mpaka akaufikia mfuko ule wa chakula, lakini ni kama mbwanae alikuwa ametambua kuwa, mtoto yule alihitaji kumuharibia rizki yake. Hakukubali pia. Tayarinae alikuwa kaufikia mfuko ule.

 Hata Maduhu alipoinua mikono yake na kuchukuwa chakula; mbwanae alifanya hivyo kitendo kilichosababisha mfuko ule uliyokuwa umebeba uchafu, umwagike chini.

 Ha! Hapo ikawa kesi nyingine. Wakati Maduhu akiparangana kuuokota mfuko ule iliaweze kutafuta wali wake, muda huohuo nd’o muda aliyojikuta akitoa ukelele mkali sana. Baada ya kuyahisi maumivu ya maji ya moto ambayo yalikuwa mwilini mwake. Hapo akabaki akilia.

 ‘’ Washenzi wakubwa nyie, kwanza nilikuwa nawatafuta sana. Na bado, tena ngoja niongeze mengine.’’ Maneno hayo aliyatamka mwanamke mmoja aliyeshikilia sufuria ambalo bila shaka lilikuwa na maji ya moto.

 ‘’ Mondesta?’’  Mwanamke yule aliita.

  Akaitika binti mmoja aliyekuwa akioshaosha vyombo.

‘’ Niletee hayo maji kwa ajili ya kunyonyolea kuku nimuoneshe huyu mtoto wa mbwa, naona yale hayajamwingia.’’ Mwanamke yule alisema, hapohapo binti aliyekuwa akiosha vyombo aliachana navyo na moja kwa moja akachukuwa jagi kisha akachota maji yaliyokuwa yameshaanza kupogoma na kumpelekea mwanamke yule.

  Mtoto Maduhu alimshuhudia mwanamke yule wakati anajiandaa kummwagia maji yale ya moto kwa mara nyingine. Hakukubali, hapo akajing’ang’aniza kuamka chini alipokuwa akiugulia maumivu na hapo akaianza safari ya kukimbia kuondoka eneo lile huku bado kilio cha maumivu aliyokuwanayo kikiendlea kumtoka. Mwanamke yule hata alipoyamwaga maji yake tayari alikuwa amechelewa kwani mtoto Maduhu alikuwa tayari ameshafika mbali kidogo, kwa ajili ya kujinusuru na maji yale ya moto.


     ITAENDELEA.
KWENDA SEHEMU YA TISA BOFYA HAPA>> SEHEMU YA TISA

0 comments:

Post a Comment