Friday, July 7, 2017


NIENDE WAPI? ‘’Dunia imenichukia’’
IMELETWA KWAKO NA SIMULIZI MIX ENTERTAINMENT                 
MWANDISHI: ZUBERY RAZUUR MAVUGO.

SEHEMU YA TISA.

ILIPOISHIA:
       Mtoto Maduhu alimshuhudia mwanamke yule wakati anajiandaa kummwagia maji yale ya moto kwa mara nyingine. Hakukubali, hapo akajing’ang’aniza kuamka chini alipokuwa akiugulia maumivu na hapo akaianza safari ya kukimbia kuondoka eneo lile huku bado kilio cha maumivu aliyokuwanayo kikiendlea kumtoka. Mwanamke yule hata alipoyamwaga maji yake tayari alikuwa amechelewa kwani mtoto Maduhu alikuwa tayari ameshafika mbali kidogo, kwa ajili ya kujinusuru na maji yale ya moto.

   ENDELEA...  ‘’ Mjinga mkubwa wewe, na unabahati... Mnakuja hapa mnatuharibia siku. Nitawamaliza mimi.’’ Mwanamke yule alifoka kisha akaachana na jambo lile na kuendelea na mambo yake mengine aliyokuwa akiyafanya hapo awali.

      Mtoto kwa jina la Maduhu muda huu alikuwa kama kichaa. Alikimbia huku na kule pasina msaada. Hakuna hata mmoja aliyemjali kila aliyemtazama barabarani aliishia kumlaani, hata wale waliyotaka kuonesha huruma mbele yake, waliyokuwanao waliwasihi.

‘’ Hivi wewe unawajua machokoraa ama unawasikia tu? Hapo ametoka kuiba nd’o maana wamemliza.’’

  ‘’ Hata kama, lakini yeye pia ni binadamu kama sisi... Vipi ateseke namna hiyo mama?’’

   ‘’ Wakati mwingine inabidi uitumie akili yako vizuri. Chokoraa ni mtu ambaye maisha yake yote yanapatikana mtaani hao nd’o majizi kama hujui. Ukisikia mtu kaibiwa sijui kabomolewa nyumba, wanaohusika na maswala hayo ni wao. Wewe si umetoka kijijini? Hujui lolote hapa mjini, ukishajangaa unaachwa kwenye mataa... Ukijifanya mama huruma, utakufa njaa.’’

   ‘’Mh! Lakini mama...’’

   ‘’ Hivi wewe mbona mbishi sana? Ayaah... Nimesahau chenji yangu kwa yule mchaga muuza nyama!’’

  ‘’ Sasa itakuwaje mama? Kama umeisahau.’’

   ‘’ Halafu kama unavyojua, hapa namuwahi shoga yangu, bado yupo nyumbani ananisubiri.’’

  ‘’ Au tuiache tutaichukuwa siku nyingine?’’

  ‘’ He! Wewe... Ushaona nani anaacha hela? Hela huwa zinasahauliwa, zikikumbukwa hufuatwa... Acha upuuzi.’’

 ‘’ Wachamie niifuate halafu wewe utangulie nyumbani, tutakutana ama unaonaje?’’

  ‘’ Hautopotea kweli wakati wa kurudi?’’

  ‘’ Hapana, siwezi mama... Nimeshapakariri, nikishuka na daladala, napandisha na kufika hapohapo.’’

 Ni maongezi yaliyoibuka kutoka kwa mama mmoja pamoja na mfanyakazi wake. Wawili wale walionekana kutoka ndani ya soko kuu huku kila ishara zikionyeshawazi kuwa, walikuwa wametoka kuhemea mahitaji fulani. Mfanyakazi wa mama yule hakuwa mkubwa, alikuwa ni binti tena mwenye miaka kumi na mmoja.

 Kama ambavyo walivyokuwa wameongea ndivyo ilivyokuwa, mama yule alitangulia na mizigo hadi kwenye daladala huku akimwacha binti yule akirudi sokoni kwa ajili ya kumtafuta mchaga muuza bucha iliaweze kumpatia kiasi cha pesa ambacho bosi wake alikuwa amekisahau.

 Alitembea huku akiangalia maeneo tofauti tofauti. Ingawa hivi sasa alikuwa na miezi kama minne tangu aingie ndani ya jiji lile la Mwanza kutoka kijijini kwao, lakini bado ushamba ulikuwa umemjaa ndani ya kichwa chake, hiyo yote ni kutokana na kutoka mara moja moja ndani ya nyumba aliyokuwa akiishi kitendo kilichompelekea ashindwe kulitambua vyema jiji lile. Hata alipofika kwa Mangi, alifanya alichotakikana kukifanya na baada ya hapo, hivi sasa alikuwa akielekea upande wa magari ambayo yangeweza kumfikisha alipokuwa akiishi.

  Akiwa katika mwendo wake mara ghafla mwili ulimsisimka baada ya kusikia sauti za kilio cha kwikwi. Macho yakatamani yajue ninini kilichokuwa kikitoa sauti zile? Kwa harakaharaka akagunduawazi kuwa, mwenye kutoa sauti ile hakuwa mbali na eneo alilokuwepo yeye, hapo kupitia masikio akajikuta akibaini kuwa, mtu yule aliyekuwa akitoa sauti zile zenyekubeba kilio cha kwikwi alikuwa amejikalia pembezoni mwa barabara. Hata alimpomtazama, hakuamini alichokiona.

 Mtoto mdogo ambaye hata yeye anamzidi umri alionekana akihangaika eneo lile. Jiraha kubwa mkononi alilokuwanalo, lilioneshawazi kwamba halikuwa likimtania bali lilimuuma kwelikweli, lakini hakuwa na chakufanya zaidi ya kulimwagia mchanga ilikuliziba dhidi ya nzi waliyokuwa wakilitamani. Kitendo kile kilimpelekea binti yule afumbe macho yake kadri alivyokuwa akilitazama jiraha lile ambalo lilikuwa likitiliwa mchanga na mtoto mwenye kutoa kilio.

 Huruma zake zikamfanya amsogelee mtoto yule kwa ajili ya kumuhoji ni kipi hasa kilichompelekea akawa namna ile? Na vipi watu wanapita kama hawamuoni ilhali yupo pembezoni mwa barabara?

   ‘’ Wewe kaka...’’ Aliita huku akimtazama mtoto yule.
 Mtoto akamtazama kwa jicho lilelile alilokuwa akilitumia kumwaga machozi yake.

  ‘’ Nini?’’ aliitika kwa mtindo huo.

  ‘’ Ha! Kumbe wewe?’’ Ni kama binti yule alimkumbuka mtoto mwenye kutoa kilio cha kwikwi baada tu yakumtazama sura.

  ‘’  Wewe nd’o nini? Na wewe unataka nini hapa?’’ Majibu ya mtoto yule yalionesha kuwa ni mtu asiye na masihara hata kidogo.

    ‘’ Wewe si yule uliyekuwa ukikimbia kule maeneo ya nje ya soko huku ukilia wewe?! Vipi, umepatwa na nini? Na mbona upo katika hali hii?’’ Binti yule alihoji.

 ‘’ We mwanamke, hebu achana na mimi... Tena sipendi mazoea na watu mie, nitakuharibu sasa hivi... Ala!’’ Alikoroma.

  ‘’ Hahahhaha... Kumbe ingawa unahitaji msaada lakini bado ni ngangari, we mtoto ukoje?’’

 ‘’ Nani unamwita mtoto? Nitakuharibia sasa hivi.’’ Mtoto yule akainuka na kushikilia jiwe lililokuwa karibu nae. Akamtazama binti yule kwa hasira za wazi.

 ‘’ Unataka kunipiga? Nipige sasa? Kwani unashindwa nini? Nipige si hata kwenu nd’o umefunzwa hivyo?  Ina maana wewe ni binadamu wa aina gani usiye na utu. Usojua kumjali mtu kistaarabu... nakuja kukujulia hali unataka kuniponda jiwe haya ponda hilo jiwe lako tuone nini utafaidikanacho.’’ Binti aliongea maneno ambayo kwa kiasi kikubwa yalimuingia mtoto yule. Hapo hasira zikamjaa kifuani.

 ‘’ Sitaki matatizo na wewe.’’ Mtoto yule akasema kisha bila kuaga akaanza kuondoka eneo lile. Binti hakutaka kukubali kumwona mtoto kama yule ambaye anaoneshawazi matatizo yamemjaa akiwa katika hali kama ile. Akajifikiria sana kisha akili ikamwambia, ‘Mfuate.’’ Binti yule akaanza kumfuatilia mtoto yule nyumanyuma huku akisahau kuwa alikuwa na safari ya kuelekea nyumbani kwao.

   Akiwa nyuma ya mtoto yule ambaye alionekana amemzidi kwa hatua kadhaa, aliweza kujifikiria sana. Ni vipi mtoto kama yule mwenye sura ya kipole awe na maneno ya ghadhabu? Ama ukali wake nd’o sababu mpaka muda huo hajaupata msaada wa aina yoyote kutoka kwa wapita njia? Na je, vipi, hana hata huruma na jiraha lake mbona anakuwa katika hali hiyo? Fikra za binti yule zikamkumbusha maneno ya bosi wake aliyezoea kumwita kwa jina la mama. Akakumbuka wakati anajuzwa kuhusiana na hawa watoto kwa jina la machokoraa jinsi ambavyo huwa walivyo, hapo akatamani akate tamaa kumfuatilia, lakini akiwa katika hali ile mara akamsikia mtoto yule akiongea.

  ‘’ Wewe mama nd’o umenimwagia haya maji ya moto hadi nikaumia hivi. Hebu ona ulivyoniunguza... Kwani mimi niikuwa na kosa gani? Nilikuja kwenye hoteli yako kufanya vurugu hadi unimwagie? Ama mimi ni mbwa?’’ Ni maneno yaliyotoka ndani ya kichwa cha mtoto yule kumfuata mwanamke mmoja aliyekuwa amekaa kwenye moja kati ya magenge yaliyokuwa eneo lile. Hapo yule binti akajikuta akivutiwa na malalamiko ya mtoto, akaongeza umakini katika usikilizaji iliaweze kujua jambo.

  ‘’ Bado umekuja eh! Yale maji ya moto hayakukuingia sawasawa, unataka mengine? Matoto yaliyotelekezwa na wazazi wao huwa yanatabu sana. Sasa kama umekoswa pakwenda, endelea kunitumbulia mimacho nikuchemshie maji mengine... Mpuuzi wewe.’’ Mwanamke yule alijibu namna ile.

  Yale majibu si tu yaliuumiza moyo wa mtoto yule wa kiume bali hata yule binti yalimuumiza pia. Ndani ya kichwa chake akaisoma jeuri ya yule mama. Akagundua sababu za mtoto yule kuwa na jiraha mkononi mwake. Kumbe alimwagiwa maji ya moto?

Uvumilivu ulimshinda mtoto yule, yaani hajaiba cha mtu halafu anaumizwa namna ile kwanini hasa? Hapo akayachukuwa macho yake mawili na kuyaangazisha chini, kisha akaanza kuyatembeza huku na kule mpaka hapo alipofanikiwa kuliona jiwe lililokuwa limeshangaashangaa mchangani, tabasamu lakujilazimisha likamtoka. Akalifuata jiwe lile kwa mwendo wa upesi, hata alipoliokota kitendo bila hata kuuliza wala kuomba ushauri kwa yeyote alilivurumisha jiwe lile hadi alipokuwa mwanamke yule.



         ITAENDELEA.
KWENDA SEHEMU YA KUMI BOFY HAPA>> SEHEMU YA KUMI

0 comments:

Post a Comment