Friday, July 7, 2017

DUKA LA ROHO SEHEMU YA NANE
IMELETWA KWAKO NA SIMULIZI MIX ENTERTAINMENT
MWANDISHI FRANK MASAI

ILIPOISHIA
 Lisa alijitahidi kuonesha furaha yake, lakini ukweli ni kwamba, hakuwa na furaha hiyo hasa baada ya kusikia mkasa ambao Frank na Malocha umewakumba kipindi hicho. Mkasa wa Jina la Chude Bobo. Walikuwa wanatafutwa kama dhahabu machimboni.

ENDELEA
Na baada ya ndoa hiyo wakaenda nchini Uswiss kula fungate lao la miezi mitatu. Baada ya kutoka huko, Gunner ndipo alipopewa taarifa kuwa mkewe anamimba yake. Jamaa alifurahi kupita maelezo na kumnunulia kila kizuri huyu mwanamke baada ya taarifa hizo za faraja kwake. Hakutaka kuhesabu muda alioutumia na Lisa katika mapenzi, alichojua yeye katundika ampendaye mimba.
Hatimaye mtoto akazaliwa na wakampa jina la Martina, jina la mama wa Lisa. Mwaka mmoja mbele, ndipo Lisa akamuacha mwanaye katika kituo cha kulelea watoto na yeye akaenda kusomea mambo ya ujasusi kwa miaka miwili.  Alipotoka, moja kwa moja akaingizwa katika shirika la FISSA wakati huo linaongozwa na Juvenile. Shirika likiwa lina uchafu mwingi kuliko shirika lolote la kipelelezi duniani. Shirika ambalo halikuwa na usawa kwa wananchi wake.
Pale Malocha alipokataa kusema ukweli kuhusu Jina la Chude Bobo, FISSA walimtuma mdunguaji wao hodari kwenda kuiangamiza familia ya Malocha.  Hayo yalifanyika kipindi Lisa yupo chuoni.
Baada ya Lisa kutoka chuoni, maisha na mumewe yakaendelea huku akiwa mtu wa kuficha siri katika ndoa yake.
Miaka minne akatimiza Martina, Gunner akawa na uhitaji wa mtoto mwingine. Bila kumwambia mkewe shida yake, akawa mtu wa kusaka mtoto huyo kwa kila hali lakini hakufanikiwa. Ndipo alipoamua kwenda kuchukua vipimo vya uzazi katika hospitali moja iliyopo nchini Afrika Kusini. Huko akaambiwa kuwa hana uwezo wa kumpa mwanamke ujauzito na tatizo hilo kazaliwa nalo. Roho ilimuuma sana Gunner baada ya kugundua kuwa analea kiumbe kisicho chake. Akarudi Tanzania na kupekua pekua nyaraka mbalimbali za Lisa na ndipo alipokutana na picha ambayo ilimuonesha Martina akiwa na miaka miwili na kwa nyuma iliandikwa "Ndoto zimekuwa kweli Man'Sai, mtoto wetu huyu.  To Frank Masai."
Ni wazi picha hiyo ilitakiwa kutumwa kwa Frank Masai wakati Martina ana miaka miwili, lakini haikumfikia mlengwa na Lisa akaihifadhi.  Mbali na picha hizo, Gunner alikuta siri mbalimbali zikiwemo za FISSA. Akajizuia asifanye chochote kwa wakati ule lakini akijiahidi kuwa ipo siku Lisa atatakiwa kuujua ukweli na atatubu. 
****** 
"Lisa, ni asubuhi mke wangu." Sauti nzito ya Gunner ilimtoa usingizini Lisa ambaye alikutana na chai nzito ya maziwa aliyoandaa mumewe. Kwa kiingereza wanaiita 'Bed and Breakfast' yaani kifungua kinywa kiandaliwachwo wakati mtu bado yupo kitandani.
"Mmmh! Swetie. Haya mambo umeanza lini tena." Lisa akamuuliza mumewe huku akinyanyua mgongo wake tayari kwa kukitafuna kile alichoandaliwa.
"Siyo mimi peke yangu. Na Martina kachangia kukuandalia." Gunner akaongea huku kagubikwa na pambo zito la tabasamu usoni pake.
"Mmmh. Miaka sita tu! Kishajua hadi ku........" Lisa hakumaliza kauli yake akaweka mkono wake mdomoni huku macho akiwa kayaweka kama mtu asiyeamini kitu fulani. Wakati huo na Gunner alikuwa kachanua tabasamu lake kama kawaida. "Ni birthday ya Martina leo." Lisa aliongea huku akimuangalia Gunner kwa hali ya sintofahamu.
"Najua majukumu ya kazi ndio yanakufanya uikumbuke birthday ya mwana wetu sasa hivi." Gunner aliongea huku bado tabasamu halimuondoki katika uso wake.
"Asante Gunner. Sijui hata nimpe nini aisee."
"Usijali, nimekwisha kuwakilisha. Na kaipenda zawadi niliyompa kwa ajili yako."
"Asante Baby." Lisa akashukuru na kumkumbatia Gunner kwa upendo wa hali ya juu.
"Labda ananipenda kwa sasa na hamkumbuki mtu wake. Ni kwa sababu sina uwezo wa kuzalisha tu! Naamini kama ningekuwa naweza kumpa ujauzito mwanamke huyu, basi sidhani kama Martina angekuwa tatizo. Ngoja niendelee kuvuta subira." Gunner aliwaza hayo kichwani wakati wamekumbatiana na Lisa.
"Kula sasa baby. Baadae nendeni mkatembee huko na Martina ili naye afurahi." Gunner aliongea hayo huku akimtoa Lisa mwilini mwake na kummiminia chai hiyo ya maziwa kwenye kikombe alichokiandaa. Lisa akatabasamu kwa furaha kwa matendo yale toka kwa mumewe.
Akaanza kunywa taratibu na vitafunwa kadha vilivyoambatanishwa na chai hiyo.
"Mamiee." Sauti ya Martina iliita kwa nguvu na kumrukia mama yake ambaye alikwishamaliza kunywa chai ile.
"Ooooh! Malaika wangu. Hujambo eeh." Lisa akamkumbatia mwanaye huku anazilaza nyuma nywele za singa alizoumbwa nazo. Nywele zinazofanana na baba yake, Frank Masai.
"Nipo salama mama. Baba kanipa zawadi, na kila siku natoka naye. Leo nataka na wewe tutoke." Martina aliongea kwa deko mbele ya wazazi wake waliokuwa wanatabasamu kwa maneno mengi ya mwana wao.
"Kwani mimi sijakupa zawadi?"
"Umenipa na nitaivaa leoleo tukitoka."
"Haya basi, kajiandae twende tukacheze cheze huko mbali." Baada ya maneno hayo, Martina alitoka nje akikimbia kwa ajili ya kwenda kujiandaa na mtoko ulioandaliwa na mama yake.
"Alikumiss sana." Gunner akimwambia Lisa.
"Nilimmiss pia. Vipi wewe, huendi na sisi?"
"Mi nitabaki. Labda twende bafuni kuoga tu! Si wajua kitambo kidogo." Gunner akichombeza na kubakiza tabasamu ambalo Lisa alilipokea kwa tabasamu pia.  Hapo Gunner akachukua jukumu la kumbeba hadi bafuni mkewe na kuanza oga naye hadi pale walipodhika. **** Ni furaha tele zilitwala katika nyuso za mama na mwana, yaani Lisa na Martina. Michezo kama bembea na kuteleza, vilikuwa vinajenga raha hiyo.
Masaa mawili yote yaliishia kwenye kucheza na kufurahi kwa pamoja, lakini hali hiyo ilikatishwa kwa simu iliyopigwa na Mubah.
"Hey Lisa. Unaweza kuja huku Kitunda." Mubah alimuuliza Lisa.
"Mmmh! Nipo Mwenge huku. Leo birthday ya Martina, nafurahi naye hapa."
"Njoo mara moja. Kuna jambo la muhimu sana nataka unisaidie."
"Okay. Nakuja. Nipe saa moja na nusu." Simu ikakatwa na Lisa akamchukua mwanaye mida hiyo ya saa tisa alasiri tayari kwenda alipoambiwa na Mubah.
Baada ya saa moja na dakika zipatazo kumi na tano, tayari Lisa alikuwa uso kwa uso na Mubah eneo la Kitunda kabla Mubah hajachukua simu ya Lisa na kuifunga kisha kuitupia kwenye ndoo ya uchafu.
Baada ya hapo, akampa simu nyingine kama ileile na kupachika kadi ambayo Lisa huitumia kuwasiliana na watu wake.
"Okay. Sasa twaweza kwenda Lisa. Lakini si kwa gari lako bali lile pale." Mubah alimuonesha Lisa gari lingine ambalo wangelitumia kwenda makao mapya ya Mubah.  Lisa akaliweka gari lake katika usalama, kisha akamchukua Martina na kwenda naye kwenye gari la Mubah bila kipingamizi.
"Hey Martina. Happy Birthday." Mubah alimtakia heri ya kuzaliwa Martina huku akimlaza nywele zake kwa nyuma wakati huo dereva wa gari hilo alishakamata njia ya kwenda Kivule.
Wakati Mubah anakamata nywele za Martina, mkono wake ukwama kwenye banio la nywele alilobania Martina.  "Hey. Kibanio chako kizuri. Umekipata wapi?" Mubah alimuuliza Martina baada ya kukiangalia kibanio hicho.
"Zawadi ya mama hii. Kanipa leo." Martina akajibu na kumfanya Mubah amtazame Lisa kwa macho ya kiulizo.
"Embu simamisha gari mara moja." Mubah akamuamuru dereva wake na yeye akatii.  "Lisa naomba tushuke mara moja." Sauti ya Mubah ikatoa ombi dogo ambalo Lisa akalitimiza na kwenda naye mbali kidogo kisha wakaanza kuteta kitu.
"Kile kibanio umempa wewe kweli?" Mubah akamuuliza swali Lisa.
"Hapana. Kapewa zawadi na baba yake. Lakini aliambiwa mimi ndiye niliyempa kwa sababu sikuwa na zawadi hii leo. Kwani vipi Mubah?"
"Hamna tatizo. Ila ni kibanio ghali sana kile, hadi nimeshtuka." Mubah alidanganya lakini ukweli ni kwamba kile kibanio alichokuwa nacho Martina, ndicho ambacho mjomba wake alipewa na Lobo. Yaani vinafanana. Ndicho kile kilichotoa sumu hatari kutoka kwenye Yellowstone.

ITAENDELEA
 KWENDA SEHEMU YA TISA BOFYA HAPA>> SEHEMU YA TISA 

0 comments:

Post a Comment