Friday, July 7, 2017


DUKA LA ROHO SEHEMU YA KUMI NA MOJA
IMELETWA KWAKO NA SIMULIZI MIX ENTERTAINMENT
MWANDISHI FRANK MASAI
ILIPOISHIA
"Ipo chini ya tajiri mmoja Mkam......" Kimya kikamkumba dada yule. Hakumaliza sentensi yake. Lisa alipomuangalia mwanamke mwenzake, alimshuhudia akidondoka kitandani kama mzigo huku damu zikimvuja kichwani palipokuwa pana tobo la risasi. Ukuta nao ulikuwa umechafuka kwa damu hizo.
ENDELEA
Yote hayo yalitokea saa mbili usiku. Kwa bastola ambayo imefungwa kifaa cha kuzuia mlio wa risasi, ikamtoa uhai mke wa Mofo.
Lisa akatazama huku na huko lakini hakuona chanzo cha risasi ile.  Akajaribu kwenda dirishani, ndipo alipoona dirisha limefunguliwa kidogo. Yeye akafungua lote na kisha akapita hapo kwa sababu kulikuwa hakuna kizuizi kikubwa cha yeye kutopita.
Alipotoka alikutana na teke zito la uso. Hajakaa sawa kiakili, akakutana tena na ngumi ya uso iliyomrudisha nyuma zaidi kimawazo. Hadi anakuja kutulia na kukaa sawa, tayari alishapokea kipigo cha maana toka kwa mtu ambaye hakumuona.
Alisikia vishindo vya kukimbia ndipo naye akajaribu kukimbia wakati huo lile eneo la nyuma kulikuwa hamna watu.
Katika kukimbia, alimuona mtu yule akimalizia kuruka geti kubwa la nyumba ile. Hapo Lisa ndipo alipoamini kuwa alikuwa hapamabani na 'kinyangala mafuta' bali chatu mwenyewe.
Naye akajitahidi kuruka na kutua nje. Akakuta mtu wake anahangaika kuwasha pikipiki aliyokuja nayo, huo ndio ukawa upenyo pekee wa Lisa kujitambulisha katika nyanja za mapigano.
Teke zito la kifuani likamkuta yule mtu na kumrusha nyuma ya pikipiki ile. Kabla hajanyanyuka, Lisa akateleza chinichini na kumkung'uta teke lingine la uso. Adui wa Lisa akadhani yataishia hapo, kumbe mwenzake ndio kwanza anayaanza.
Sarakasi mbili za kujibetua kwenda nyuma, zikapigwa na Lisa, kisha akamaliza kwa kujitupa kwenye tumbo la adui yule. Hapo akasikia sauti kali ikitoka kwenye kinywa cha mtu yule.
"Kumbe ni mwanamke." Lisa akajikuta akiropoka baada ya sauti ile. Kwa mavazi ya kininja aliyovaa mtu yule, ni ngumu kujua anajinsia gani. Baada ya kipigo akajitambulisha kwa mlio huo wa kike.
Lisa akajisahau kidogo na huo ndio uliokuwa wasaa wa yule adui kupitisha miguu yake shingoni kwa Lisa na kisha kumkaba kwa nguvu bila kumuachia. Kila Lisa alipojaribu kufurukuta, hakuchomoka na badala yake, roba ikawa inazidi kumbana hadi akasaliti amri kwa kuzimia palepale.
Hapo yule Mwanamke ninja, akawahi pikipiki yake na kuipa kiki ya nguvu, nayo ikakubali sheria. Mwendo wa ajabu ukachukua nafasi yake baada ya kuwaka. Akaondoka eneo hilo huku akimuacha Lisa hana fahamu. **** "Lisa, Lisa, Lisa." Sauti ya mwangwi ilisikika kwenye kichwa cha Lisa. Akajaribu kufumbua macho na kuona nani anamuita. Ilikuwa ngumu kwake kurudiwa na fikra zake lakini alijitahidi na kufanikiwa kufungua milango yake ya fahamu.
Sura za rafiki au wafanyakazi wenzake aliziona zikiwa zinamtazama. Akatulia dakika kama tatu kisha akafyonza baada ya kukumbuka tukio zima lililotokea nyumbani kwa Mzee Rofo.
"Mbwa yule ni kweli hayupo peke yake. Leo nimepambana na mwanamke mwingine." Lisa aliongea huku akinyanyuka kwenye kitanda ambacho alikuwa kalazwa.  Ni katika nyumba ileile ya Kivule ndipo aliporudishwa tena.
"Vipi hali yako lakini?" Malocha alimuuliza Lisa.
"Nitakuwa vizuri. Martina yupo wapi?" Lisa akamkumbuka mwanaye.
"Yupo chumba cha mapumziko kalala." Akajibiwa.
"Kwani sasa hivi saa ngapi?"
"Ni saa nne hii."
"Oooh! Mungu wangu. Sijui mume wangu atakuaje."
"Usijali tumempa taarifa kuwa upo kwetu na utarudi kesho." Lisa akapumua pumzi ya ahueni kisha akatulia kitandani na kuanza kusimulia mkasa mzima ambao ulimtokea.
"Daah! Hawa watu si wa kuchezea kabisa. Wapo vema kila idara. Hapa cha msingi ni kujitahidi kucheza na silaha." Mubah alitoa ushauri kabla hawajamuacha Lisa peke yake mle chumbani.
"Sasa kama ulivyoona, tumepoteza chanzo kingine. Hapa tumebaki na hicho kibanio tu! Tumejaribu kufuatilia vinapotoka, tumegundua ni Malyasia. Huko itabidi uende peke yako Mubah." Malocha alikuwa akimpa mchakato mwingine wa kufanya Mubah.
"Mmmh! Mkuu, kwa nini tusimwambie ukweli Lisa ili tushirikiane naye kupambana? Wajua siwezi peke yangu. Tumwambie tu ukweli." Mubah alitoa ushauri ambao Malocha aliinamisha kichwa chake chini kabla hajatoa maamuzi.
"Wajua ni ngumu sana. Halafu maisha ya Lisa tutayaweka matatani zaidi." Malocha akatoa jibu.
"Lakini hata hivyo siku akijua tayari maisha yake yatakuwa hatarini." Mubah aliweka neno ambalo nalo halikuwa baya.
"Okay. Tutamwambia. Lakini siyo leo wala kesho. Hiyo ni kwa usalama wa.mwanaye zaidi." Malocha aliongea.
"Kwani mtoto naye ana nini. Mtoto wao halafu wamdhuru?" Mubah akapatwa na mshangao. Malocha akamsogelea Mubah pale alipo kisha akaanza kwa kumgonga gonga bega.
"Jambo usilolijua, ni sawa na usiku wa kiza. Tuyaache hayo, nishatoa neno na litimizwe. Utaenda Malyasia." Malocha akamaliza.
"Sitaenda kama huwezi kumwambia ukweli Lisa. Lisa yapaswa aambiwe ukweli." Mubah alimfata mkuu wake na kumwambia maneno hayo kwa msisitizo.
"Mnataka kunificha nini?" Lisa akatokea na kuwauliza Malocha na Mubah huku akiwaangalia kwa zamu. "Mnataka kunifanya na mimi ni mtoto mdogo? Niambieni mlicho kificha. Yawezekana hata yule mtu aliyemuua mke wa Rofo mlinitegea nyie. Tangu natoka pale Kitunda, huyu alikuwa ananiangalia kwa mashaka. Sasa nataka mniambie ukweli sasa hivi." Lisa akaweka mkazo kwenye akitakacho huku sauti yake ikiwa katika hasira.
"Lisa tulia. Kila kitu kitakuwa sawa. Na kila....." Hakumaliza kauli Malocha, ikawa imekatwa na Lisa.
"Sitaki maelezo ya kipumbavu kama hayo. Nataka muwe straight katika majibu nayoyataka. Nini mnanificha?"
"Mume wako anashirikiana na Lobo." Malocha akamwambia Lisa na kuondoka lile eneo huku akiwa kakunja sura yake.  Akabaki Mubah ambaye alikuwa akimtazama Lisa aliyekuwa katika mkanganyiko wa hali ya juu baada ya maneno yale.
"Haiwezekani." Lisa akatamka hayo huku taratibu akishuka na kujikuta akikaa chini.
"Ni kweli Lisa. Na ndiye niliyemuona mara ya mwisho kabla sijazimia ile juzi wakati nyumba yangu inalipuliwa." Mubah alichomelea ukweli ambao anaujua. "Na hata hicho kibanio cha mwanao, kinafanana na kile ambacho kilitema sumu na kuua wenzetu kule nyumbani. Na yewezekana yule mtu uliyepambana naye, kakuacha sababu ya ukaribu wako na Gunner." Mubah akamaliza huku naye akienda na kukaa pale alipokaa Lisa.
"Yawezekana ile picha ya Martina aliyonionesha Lobo wakati tumemkamata, kampa yeye Gunner. Kama kampa yeye, basi tayari anajua siri nyingi sana zituhusuzo." Lisa akaamua kufunguka.
"Ni kweli. Kakuwekea GPS katika mifuko yako mingi unayokuja nayo kazini. GPS hizo ni ngumu kujulikana pale unapokaguliwa na vifaa vya FISSA kwani GPS hizo ni za plastiki na hazitumii aina yoyote ya umeme." Mubah akamtobolea ukweli uliokuwa mgumu kuamini kwa yeyote mwenye mapenzi.
"Okay. Sasa naanza kupata picha kwa nini anamfundisha Martina kutumia silaha. Mjinga sana yule, kesho naenda kumuua." Lisa aliongea kwa kiapo na kunyanyua uso wake ambapo alikutana na uso wa Malocha ukiwa unamtazama kwa makini.
"Lisa. Hata ukipewa miaka ishirini ya kumuua Gunner, hutoweza. Yule umuonavyo, sivyo alivyo. Ni heri ukutane na treni ya umeme relini, kuliko kukutana na uso halisi wa yule mtu. Tutakupoteza dakika sifuri tu." Malocha alimtahadharisha Lisa kwa maneno machache.
"Sasa nifanyaje?" Lisa alimuuliza Malocha.
"Cha msingi ni wewe kutulia hapa. Hatofika mtu hapa. Au kama waweza, rudi kwako na kujifanya hujui lolote. Na kingine, mtoto wako anafundishwa kulenga huku akioneshwa picha ya Frank." Malocha akamaliza na kuelekea chumba kilichokuwa na mitambo ya kipelelezi.

Akamuacha Lisa akiwa kakodoa macho asijue ni nini afanye kwa wakati ule. Mubah naye akanyanyuka na kuondoka eneo lile akiwa na amani kiasi baada ya Lisa kuugundua ukweli.

ITAENDELEA

KWENDA SEHEMU  YA KUMI NA MBILI BOFYA HAPA=> SEHEMU YA KUMI NA MBILI 

0 comments:

Post a Comment