Thursday, July 6, 2017

DUKA LA ROHO SEHEMU YA SITA
IMELETW KWAKO NA SIMULIZI MIX ENTERTAINMENT
MWANDISHI FRANK MASAI

ILIPOISHIA
Miili minne, akiwepo na yule mtoto ambaye walimfanya kama mjomba wa Muba ilikuwa imelala kifudifudi kwenye viti walivyokalia huku moshi mdogo ukiwatoka midomoni mwao. Nyuso zao zilijikunyata na kuwa kama za wazee wa miaka mia moja. Damu ilikaushwa katika miili yao kwa kutumia sumu kali inayosambaa kwa hewa.
Mubah alipoangalia sehemu alipokanyagia kile kibanio, alikuta kuna majivu machache ambayo yalitokana na kile kibanio kuungua.
  
ENDELEA
"Nadhani umeona. Sikutaka kukuua wewe. Na hata hicho kimdoli mlichokifanya ni kitoto kidogo, nacho kingekuwa na uhai, ningeua tu! Na nitakiua hichi nilochonacho huku baada ya dakika tatu kupita." Lobo aliongea kwa sauti iliyojaa chuki. "Hiyo sumu inatoka kwenye madini ya yellowstone. Madini yafananayo na almasi sema yenyewe ni ya njano na yanayeyuka. Husambaa kwa sekunde thelathini baada ya kuchomwa moto na hupotea kwa sekunde kumi na tano baada ya kusambaa. Kibanio hicho nilieweka jiwe dogo sana la madini hayo. Na nilitega kifyatulio ambacho kikifyatuka, hutengeneza moto. Nimefanikiwa hilo Mubah, asante kwa kuniletea wateja hao. Bado dakika mbili." Lobo akamaliza kuongea na kuacha simu hewani ili asikie upande wa pili.
"Nooooooo. Don't do that Lobo. Please." Mubah alijikuta akipiga kelele ya nguvu huku akijaribu kuomba msamaha.  Kelele hizo zikawafikia walinzi wa nje nao wakakimbilia ndani wote, hata wale wadunguaji nao ikabidi kushuka kule juu haraka na kwenda ndani kutazama kile kinachoendelea. Walichokikuta ndani, hakika kiliwatoa machozi na kuwaacha katika mshangao. Sasa hivi miili ile ilikuwa ikipukutika kama majivu ya karatasi na mwisho wake yakabaki mafuvu yamekaa kwenye viti.
"Sasa naweza kukusikiliza Mubah, unadakika moja. Toka nje na mtu yeyote asikuone kama umetoka. Nataka nikuoneshe kitu." Sauti ya Lobo ilisikika ikimuongelesha Mubah kwenye simu.  Mubah akafanya kama alivyoambiwa.
"Sogea mbali na nyumba yako. Na itazame kwa macho ya umakini, utaona kitu cha kukupendesha. Zimebaki sekunde kumi na tano muda wetu uishe." Lobo alitoa ombi ambalo Mubah alilifanya haraka na kukazia macho yake kwenye nyumba yake ambayo ndani yake kulikuwa na wafanyakazi wenye uhai wapatao kumi na moja.
"Tano, Nne, Tatu." Lobo akaanza kuhesabu sekunde zilizobaki hadi akafikia moja, kisha sifuri.  Macho ya Mubah yakajawa na taharuki ya ajabu. Hakuwahi kufikiria katika maisha yake kuwa kuna siku atashuhudia kile anachokishuhudia kwenye nyumba yake. Alishazoea ni kwenye filamu za kivita tu! Ndio awezapo kuona yale mambo.  Lakini sasa anajionea kwa macho yake yale ambayo alikuwa anayaona kwenye filamu.
Nyumba yake ililipuka yote na kuteketea kama vile uonavyo kwenye filamu ndege au meli inapopigwa bomu. Nyumba ikazidi kuteketea na kuteketea hadi vile vilivyomo ndani.
Mubah akapiga magoti na kulia kwa sauti huku akipiga chini ngumi kadhaa lakini bado hakukuta simu bali kusikiliza kilichokuwa kinataka kujiri.
"Woooou. I like that sound of boom, yoo. (Waau. Nimeipenda hiyo sauti ya buum, yoo)" Lobo alisikika akiongea hayo kwenye simu baada ya ule mlipuko mkubwa kutokea kwenye nyumba ya Mubah.
"Please Lobo, naomba uiache familia yangu. Nakuomba Lobo, nitaacha kazi kama utakavyo." Mubah akikuwa anaomba msamaha huku kapiga magoti katikati ya barabara ya lami iliyokuwa inapitwa watu huku na huko kukimbia ule mshikemshike wa bomu.
"Too late Mubah. Umechelewa mwenyewe kufanya chaguo lililo sahihi na mimi huwa sikwepeshi kauli yangu." Lobo aliongea hayo na hapohapo sauti ya 'kitoto kichanga' ikaanza kulia.
"Muache mwanangu we kafiri. Na kwambia muache." Sauti ya dada wa Mubah ilisikika na kupenya kwenye ngoma za Mubah. Wakati huo sauti ya. kichanga iliendelea kulia na mara ikakata ghafla baada ya mlio mkali wa bastola kutoka.
"Nooo." Sauti ya dada wa Mubah ilisikika mara moja na baada ya hapo haikusikika tena. Lobo akiwa anachalaza mluzi usioeleweka ni wa wimbo gani, akaongea kwenye simu ambayo Mubah alikuwa bado hajaikata.
"Dada yako kazimia baada kuona mwanaye mdogo nikitoboa kichwa chake kwa risasi yangu. Hahahahaaa. Nasikitika hutoona maiti zao kwa macho yako bali utaona picha za maiti yao. Naua na kupiga picha." Lobo alimpa taarifa Mubah ambayo ilimzidishia maumivu moyoni.
"Lobo tafadhali, nisamehe. Kuwa na utu we' mtu. Naomba uniachie familia yangu." Mubah aliongea kwa sauti ya kitetemeshi iliyojaa kilio.
"Ankoo tuokee." Sauti ya mjomba kipenzi wa Mubah ilisikika.  Mubah akahisi mwenye kutaka kufa lakini hakufa bali alizidi kushikilia simu yake sikioni.
"Anko kwa heri. Labda tutakuja kuonana tena. Nakupenda sana ank....." Yule mjomba wa Mubah hakumaliza kuongea kitu akamezwa na mlio wa bastola ya John Lobo na hapohapo hakusikika tena. Mubah alilia kwa sauti ya juu ambayo ilimfanya adondoke kwenye lami alipokuwa kapiga magoti na wakati anadondoka, akaliona gari moja jeusi likipita karibu yake na mtu aliyekuwamo mle ndani, alimuangalia kisha akatabasamu kwa tabasamu pana kabla hajafunga kioo cha upande wake kilichokuwa cheusi. Sura ile ya kiume haikuwa ngeni kwake, lakini alisahau kaiona wapi. Na wakati huo alikuwa hana nguvu zozote za kuinuka pale alipo ili akimbize lile gari. Badala yake, alilala pale chini taratibu huku akianza kuona giza likitanda usoni pake.
"Huyu nimeingiza bastola mdomoni na kufumua ubongo wa nyuma kwa bastola yangu. Ha ha haaa raha sana kuua." Hiyo ndiyo sauti ya mwisho ya kutoka kwa Lobo ambayo Mubah aliisikia.  Fahamu zikapotea kwa sababu ya machungu tele yaliyojengeka moyoni mwake.
****
 Ilichukua karibu saa moja kwa Mubah kuamka na kushtuka tena baada ya kukumbuka yale ya nyuma. Tayari alikuwa yupo ndani ya FISSA baada ya wafanyakazi wenzake kuja kumuokota pale chini alipokuwa kazimia.
"Husna, Husna, Husna, Husnaaa. Kweli umeenda uncle wangu niliyekupenda kuliko wote nyumbani? Nitacheka na nani tena, nani atanifurahisha pale niwapo na machungu. Ooh! Mungu wangu nisaidie." Mubah alikuwa akilia kwa uchungu mbele ya wafanyakazi wengine ndani ya FISSA.
"Nyamaza Mubah. Pole sana. Hakuna ambaye hana hayo machungu. Tuliizoea familia yako na tuliwazoea wafanyakazi wetu, lakini wote hatunao tena. Inatuuma sana." Dada mmoja mrefu na mweusi lakini mwenye mvuto wa aina yake, alijaribu kumbembeleza Mubah aliyekuwa akilia kama mtoto mdogo.
"Atalipa tu huyu mbwa. Nitamuua kwa risasi zangu. Nitamuua Lobo na washirika wake wote. Nishamuona mmoja, nitamsaka na kumuadhibu pumbavu yule." Mubah aliongea kwa hasira huku akinyanyuka katika kitanda cha dispensari iliyopo mlemle ndani ya FISSA. Akashika kitasa cha mlango wa kituo kile cha afya na kutoka humo kituoni na kuanza kuelekea ofisi za kipepelezi hasa kule zinapokaa kamera maalumu za kufatilia mienendo yote ya kazi za FISSA.
"Niwekee mkanda wenye tukio zima la pale nyumbani." Mubah aliongea mbele ya mwanakaka mmoja aliyekuwa anacheza na kompyuta za mle. Yule jamaa hakuwa na kipingamizi hasa kwa kuwa ule mkanda unamgusa sana aliyemuamuru auweke. Akauweka na kisha ukaanza kucheza matukio yote yaliyokuwa yanaendelea siku hiyo kabla Mubah hajazimia. Mkanda huo ukaenda hadi mahali ambapo nyumba ya Mubah ilipolipuliwa.
"Rudisha hapo kidogo." Mubah akamwambia maneno yale yule opareta. Jamaa bila ubishi akarudisha sehemu ambayo inaonesha nyumba ya Mubah ndio inataka kulipuka.
"Umeona hapo?" Mubah akaonesha kwa kidole sehemu husika anayotaka yule opareta aione. Opareta akatazama kwa makini, alipoona kama hapaoni, akapavuta kwa ukaribu kisha akatoa mawimbi ambayo yanasababisha picha isionekane vema.
"Okay. Hili ni bomu toka kwenye RPG hili." Opareta akaongea baada ya kugundua hilo jambo.
"Sasa kumbe John Lobo hayupo peke yake. Wakati nyumba hii inalipuka, mimi nilikuwa naongea naye na alikuwa na familia yangu mbali na pale nyumbani. Lazima tuwasake hawa washenzi." Mubah aliongea kwa hasira na kukita ngumi nzito kwenye meza iloyomo mle ndani. Kwa hasira akageuka nyuma na kutaka kuanza kutoka lakini baada ya kugeuka, akakutana na sura ya Malocha.
"Mubah. Unatakiwa kupumzika kwa miezi miwili. Hii kesi tuachie sisi, tutaimaliza tu!" Malocha alimwambia Mubah ambaye alimtazama kwa jicho kali na la ghasia.
"Huu ushauri ungenipa kabla familia yangu haijaondoka duniani. Ungeniambia niache kazi kabisa ili familia yangu ipone, lakini siyo sasa hivi. Nitapigana kufa na kupona ili huyu mbwa nimkamate. Nimeshajua hayupo peke yake, nitamsaka tu!" Mubah alimueleza Malocha na kumpita pale aliposimama kwa kutaka kutoka ndani ya ofisi ile. Lakini Malocha akamkamata mkono na kumrudisha mbele ya upeo wa macho yake.
"Nilipoteza familia yangu kwa mkono wa huyuhuyu Lobo. Kwa risasi tano alizopewa, hakumkosa yeyote katika familia yangu. Nilijawa na jazba kama wewe hivyo, nikapania kumuua na nilifanikiwa kukamatiwa huyu mtu, nikawa naye uso kwa uso akicheka kwa dharau. Nilikata shingo yake, kisha nikamvunja miguu kwa risasi mbili na tatu nikamchapa nazo kifuani (MKASA HUU UPO KWENYE RIWAYA YA JINA). Nikadhani amekufa, lakini leo hii tunapambana naye tena. Naona ni kama mzimu au shetani ambaye hafi, au jini. Lobo huwezi kupambana naye peke yako na ukashinda vita yake. Utapotea Mubah." Malocha aliongea kwa makini na kwa upole huku machozi yakiwa yanataka kumtoka kwa mbali.
"Baada ya kupoteza familia yako, ukamsaka na kumpata kisha ukamuua. Niachie na mimi, nimepoteza familia yangu, nimsake nimpate kisha nitakuletea kiwiliwili chake." Sauti ya kujiamini toka kwa Mubah ilipenya masikioni mwa wale wanaofatilia yale maongezi, akiwemo Malocha.
"Nimekwisha kwambia, acha hiyo kesi. Ni amri siyo ombi. Nakupa miezi miwili ya kupumzika, utake usitake, utaenda mapumziko." Malocha ikabidi atumie nguvu za uongozi wake kuwasilisha hisia zake. Mubah akatulia kwa muda kabla hajarudi kwa yule opareta na kuchukua ule mkanda wenye tukio zima la siku hiyo.

ITAENDELEA...

KWENDA SEHEMU YA SABA BOFYA HAPHA>> SEHEMU YA SABA

0 comments:

Post a Comment