Friday, July 7, 2017


NIENDE WAPI? ‘’Dunia imenichukia’’
IMELETWA KWAKO NA SIMULIZI MIX ENTERTAINMENT                          
MWANDISHI: ZUBERY RAZUUR MAVUGO.

SEHEMU YA KUMI NA MOJA.
    
ILIPOISHIA:
     Alipoagana na mkewe akatoka, na moja kwa moja akaelekea kwenye kituo cha daladala, hata alipofika alipanda magari yaelekeayo mjini. Yalimtua na yeye akaanza safari ya kulifuata soko kuu. Alipofika ndani ya soko hilo alielekea upande wa wauzaji wa kuku na moja kwa moja akawafuata mabwana watatu waliyokuwa wamesimama pembeni kidogo, akawasalimu na wao  wakamwitika kama kwamba wanafahamiananaye kisha, wakamlaumu kwa kuchelewa, alizikubali lawama zile na mazungumzo yakaanza.

  ENDELEA... Mazungumzo yao hayakuonekana kuhusisha jambo jingine zaidi ya biashara. Mwisho wa siku walielewana na bwana Mashaka akaachwa pale yeye pamoja na mabanda kadhaa ya kuku ambayo ndani mwake yalihifadhi kuku wakubwa kwa wadogo.

   Akiwa mwenyewe aliwafuata wauza kuku majirani zake na kuanza kuwaulizia mambo kadha wa kadha aliyoyajua mwenyewe.

‘’ ... Vizuri, nashukuru sana. Mie kwa majina naitwa Kijogoo Hasani... Karibu sana.’’

‘’ Ahsante, nami pia nashukuru kukufahamu.’’

  Walipomaliza kusalimiana alihoji maswali kadhaa aliyohitaji na kupatiwa majibu yaliyomridhisha. Hadi anatoka pale tayari alikuwa amesha jifunza mengi sana; Kujifunza kwake haikumaanisha kuwa wazo la kuku katika maisha yake ni la jana ama leo. Kiufupi lilikuwa moja kati ya mawazo yaliyosahaulika. Akikumbuka mshawishi mkuu wa jambo lile alikuwa ni baba yake mzazi, mzee Magabe.

  Mzee aliyekubali kuitwa kila aina ya majina ilimradi aziheshimu nywele zake. Hakujali walipomuita manyewele, alichojali ni kuhakikisha ana acha pesa kila siku nyumbani kwake na watoto wake wanapata kusomo, ingawa alikuwa ni mtu wa watu lakini alikuwa na mawazo binafsi ya kimaendeleo. Kila siku jioni alimwita manae mkubwa wa kiume kwa jina la Mashaka na kumtoa kando kidogo kisha alimweleza nini maana ya maisha na ni vipi kijana anapofikia umri wa kujitambua anapaswa awe.

 Laiti kama kuna mtu mwingine angekuwa akiyasikia maneno ya mzee Magabe dhidi ya mwanae, kiukweli angehisi huenda mzee yule ameshachizika. Alifanya yote hayo huku akiamini na kumwambia mwanae kuwa, ‘ Hatuyajui ya kesho, hata sasa naweza kuondoka duniani ukakosa baba wa kukupa maarifa.’  Mashska aliyatii maneno ya baba yake na kufuata kila alichoambiwa.

 Naam, hata hivyo Mashaka alisoma na kumsaidia haswa baba yake, ukija katika swala la uuzaji na ufugaji wa kuku, hakuwa mtu mwenye uwezo wa kawaida. Alipomtazama kuku fulani aligundua mpaka mambo yanayoweza kumfanya akapatwa magonjwa, udhaifu wake baada ya magonjwa na kadha wa kadha. Kitendo hicho kilimpelekea hata kuwa bora shuleni na kujiingiza kwenye krabu mbalimbali za ujasiriamali ambako huko pia alijifunza mengi sana.

  Alijipatia elimu ya kutosha kutokana na kazi ile ya baba yake mpaka hapo alipoamua kujitegemea baada ya kupata kazi nzuri yenye malipo ya kufaa. Muda kidogo alipotoka kwao, baba yake nae hakukawia, mapafu yaliyokuwa yakimsumbua kwa muda mrefu nd’o hayo yaliyomuondoa duniani.

  Tangu alipopata kazi na kupata pesa, alijikuta akizisahau kabisa ndoto zake za kufuga na kuuza kuku. Akajidanganya na kuiamini benki kuliko chochote maishani mwake huku akijua kununua nyumba na magari ndivyo vitavyomfanya awe tofauti na hata kuendelea kwenye maisha mazuri, hakujua kama kufumba na kufumbua, pesa zilizo kuwa benki zinaweza kuchukuliwa zote na hata kumfanya awe mtu asiye na mbele wala nyuma. Baada ya kuteseka mtaani, hapo ndipo alipoyakumbuka yale mawazo ya baba yake, alitamani aanzishe mradi wa ufugaji kuku na hata kujiingiza kwenye uuzaji kuku lakini hakuwa na pesa.

 Hata alipofanikiwa kuzipata pesa zile ndipo alipoamua kucheza na akili yake kwa haraka, na kuanzisha mradi wa uuzaji kuku huku akiwaza endapo kipato kikieleweka basi atajitupia katika ufugaji, awe kama marehemu baba yake.

  Hivi sasa alikuwa akishughulika na wateja. Atoke huyu aingie yule yote hiyo ni kutokana na kuuza kuku wa haja! Biashara alijikuta akiifurahia ingawa nd’o kwanza alikuwa akianza, hata jioni ilipofika alifunga banda lake na kuagana na wauzaji wenzake kisha akaianza safari ya kurejea nyumbani kwake.

 Alipofika alimkuta mkewe akiwa amejilalia kwenye kochi huku akitazama televisheni.

 ‘’ Vipi mbona umeondoka tangu muda ule mpaka sasa? Ulikuwa wapi?’’

 ‘’ Nilikuwa kazini?’’

  ‘’ Ha! Mume wangu? Kazi gani tena? Au umeshasahau kama wewe huna haki ya kufanyakazi kutokana  na yaliyotukuta.’’

  ‘’ Mke wangu, sifanyi kazi ndani ya kampuni, nipo mimi kama mimi... Hivi sasa nafanya kazi ya kuuza kuku.’’

 Waliongea mengi sana, mkewe alifurahi sana baada ya kusikia jambo lile kutoka kwa mumewe, hapo akaanza kumuuliza mambo kadha wa kadha kama mipango na malengo ambayo mumewe amejiwekea.

  ‘’ Sasa ni vyema ungepata maji ya kuoga kwanza.’’ alisema na mumewe akaafiki.

 Usiku huo waliufurahia kwa utani wa hapa na pale, mambo haya na yale. Wakikumbuka maisha waliyopitia baada ya kufukuzwa kazi, aibu walizozipata kiasi cha kutothaminiwa na yeyote, hapo waliishia kusema, ‘Fadhili mbuzi utakunywa mchuzi binadamu atakuudhi’ na misemo mingine mingi yenye maana kama hiyo ama zaidi yake.

   ***

Bado aliendelea kurandaranda mitaani kama kawaida yake. Kila alliyepita katika mtaa ule yeye alimpiga jicho na hata kumchunguza kutumia sayansi yake aliyeiita ‘sayansi ya kujikimu.’ Hakuwa na mtaji wowote ule zaidi ya yeye mwenyewe. Siku hiyo ni kama ilikuwa ya manyanyaso kwake, mpaka usiku ule ni vipi hajapata windo hata moja?

 Akiendelea kutafakari kwa uchungu mara alimwona bwana mmoja mwenye tumbo kubwa, aliyevalia suti ya haja, huku simu ya kugusa kwa kidole ikiwa mkononi mwake, akionekana kama mwenye kuwasiliana na mtu kwa njia ya ujumbe ama mwenye kuperuzi.

  Mwindaji yule hapo kidogo roho ilimtulia akajihisi amani na kuanza kulifuatilia windo lake. Ingawa alilihofia umbo la bwana yule kutokana na yeye kuwa mdogo lakini alijikuta akitabasamu baada ya kumtazama sura yake.

  Alitamani kucheka lakini akajikaza. Bwana mwenye umbo nene alikuwa na sura yenye kuwiana  na mtoto mchanga isiyo na kovu wala nini? Tangu lini mtoto yule kwa jina la Maduhu aogope watu wenye sura za kitoto? Hapo akaingiwa na imani l kwamba; lazma angeimiliki simu ile na kuitafutia mteja huku yeye akipata pesa ambayo ingemwezesha kupata chakula.

 Hata bwana yule mwenye sura ya mtoto mchanga alipomkaribia hakumjali maana hakujua chochote kilichokuwa kikiendelea, mara kufumba na kufumbua akajikuta hana simu mkononi mwake. Baada ya kutazama ndipo alipomuona mtoto mdogo akikimbia kuelekea vichochoroni. Hapo akatamani kumfuata, akiwa njiani akakumbuka jinsi ambavyo kumfuata mtoto yule kunaweza mfanya hata ayahatarishe maisha yake.

 Kwani simu kitu gani juu ya uhai? Akili yake ilimwambia na hapo akaamua kuachana na mtoto yule kisha akaendelea na safari zake.

 Jambo lile lilikuwa kama dharau na kashfa mbele ya kijana Maduhu; ni wazi kuwa, hajazoea kukwapua cha mtu na kutelekezwa bila hata kutimuliwa. Alihisi huenda mtu yule mwenye sura ya mtoto mchanga alikuwa akimjaribu, lakini aliziondoa hisia zile baada ya kukumbuka kuwa, ndani ya dunia hii kuna watu kwa jina la matajiri.

 Maadam yupo hai, hakuhitaji kuyajali sana maswala hayo, akajipitisha sehemu tofauti tofauti zilizo changamka ndani ya jiji hilo. Hapo akafika kwenye duka moja la simu na kukutana na muhudumu aliyeonesha kufahamiana nae.

  ‘’ We mduanzi, hii kitu ina shilingi ngapi hapo dukani kwako?’’

  ‘’ Kitu ina lakini na nusu hii.’’

  ‘’ Basi shega... Bunda, tutakutana baadae.’’

 Baada ya maneno hayo machache akatoka ndani ya duka lile la simu na kuelekea kwa jamaa yake mmoja mrusha miziki. Wakasalimiana kwa salamu zao kisha akamwelezea kuhusu simu ile na kumwambia endapo atamtoa shilingi elfu ishirini tu basi kila kitu watakuwa wamemaliza. Rafiki yake yule hakutaka hata kuuheshimu uzuri wa simu ile, hapo badala aombe, yeye akashusha bei na kung’ang’ana apewe kwa shilingi elfu kumi simu ile ya laki na nusu.


     ITAENDELEA.

KWENDA SEHEMU YA KUMI NA MBILI BOFYA HAPA=> SEHEMU YA KUMI NA MBILI

0 comments:

Post a Comment